WAZIRI MKUU THAILAND AGOMA KUJIUZULU



Thailand’s Prime Minister Yingluck Shinawatra
Waziri Mkuu wa Thailand, Yingluck Shinawatra


Waziri Mkuu wa Thailand, Yingluck Shinawatra amekataa kujiuzulu kwa madai kuwa wito unaotolewa na waandamanaji wa kumtaka kufanya hivyo sio wa kikatiba.

“Ninaweza kufanya chochote kwa ajili ya kuwafurahisha wananchi wangu, nina utashi wa kufanya hivyo, lakini kama waziri mkuu, kila ninachokifanya lazima kiwe ndani ya katiba,” amesema waziri mkuu huyo katika hotuba yake kwa taifa lake.

Jana kiongozi wa upinzani, Suthep Thaugsuban, alitoa muda wa mwisho wa siku mbili kwa bibi Yingluck ajiuzulu na “kuyarejesha madaraka kwa wananchi.”

Waziri Mkuu alijibu na kusema kuwa takwa la kuhamisha madaraka kutoka kwa waziri mkuu aliyechaguliwa kidemokrasia na kuyahamishia kwa wananchi “halipo chini ya sheria ya katiba.”

Waandamanaji nchini humo wanaipinga serikali ya Yingluck Shinawatra, ambaye ni dada wa waziri mkuu wa zamani Thaksin Shinawatra  aliyeondolewa madarakani katika mapinduzi ya mwaka 2006. Thaksin, ambaye anadaiwa kuwa na mkono wa nyuma ya pazia kwenye serikali ya sasa, amekuwa akiishi uhamishoni tangu alipong’olewa madarakani.

Aidha, Yingluck alieleza kuwa jeshi la nchi hiyo halitaegemea upande wowote na anajua vyema kwambwa wanataka kuona nchi ikiwa katika amani.

Kwa mara nyingine, polisi wamekabiliana na waandamanaji hao wanaoipinga serikali, ambao wanajaribu kuyazingira na kuyakalia majengo ya serikali ikiwemo ofisi za Baraza la Mawaziri la nchi hiyo lililopo mjini Bangkok. Polisi wametumia gesi ya kutoa machozi, risasi za mpira na maji ya kuwasha katika kuwatawanya.

Waandamanaji hao wameshayashikilia majengo kadhaa ya serikali ikiwemo jengo la wizara ya fedha.

Kiasi cha askari 3,000 wa usalama wamewekwa kwenye ofisi muhimu za serikali.  

Maandamanaji hayo yalishtadi mwishoni mwa juma baada ya waandamanaji wanaoiunga mkono serikali, wanaojulikana kama “fulana nyekundu”, walipofanya maandamano kuonesha uungaji mkono kwa serikali ya bibi Yingluck.

Ripoti zinasema kuwa watu kadhaa wameuawa na wengine wengi kujeruhiwa katika maandamano ya hivi karibuni yaliyoutikisa mji mkuu, Bangkok.

Viongozi wa maandamano wanatoa wito wa kufanyika kwa mgomo wa nchi nzima katika jaribio la kuishinikiza serikali kujiuzulu.


Maandamano nchini humo yaliibuka pale bunge la seneti lilipoukataa muswada wa serikali ambao ungetoa msamaha kwa waziri mkuu aliyetimulia, Thaksin Shinawatra na kumuwezesha kutoka uhamishoni na kurejea nchini. 
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment