WAZIRI MKUU WA ETHIOPIA AJIUZULU

 Ethiopia prime minister Hailemariam Desalegn resigns


Waziri mkuu wa Ethiopia, Hailemariam Desalegn, amesema kuwa amewasilisha barua yake ya kujiuzulu wadhifa wake wa Uwaziri Mkuu na uenyekiti wa muungano wa vyama vinavyotawala nchini humo.


Tangazo la Hailemariam linakuja huku kukiwa na mzozo wa kisiasa na ghasia katika taifa hilo la pembe ya Afrika, ambalo limeshuhudiwa kuachiwa huru kwa maelfu ya wafungwa wa kisiasa ili kutuliza hali ya mambo.


"Ukosefu wa utulivu na mzozo wa kisiasa vimesababisha kupotea kwa maisha ya watu na wengi kukosa makazi," alisema Hailemariam katika hotuba yake iliyotangazwa kwa njia ya televisheni.


"Suala la kujiuzulu naliona kama hatua muhimu ya kuendeleza mageuzi yatakayopelekea kuwepo kwa amani thabiti na demokrasia," alisema.


Hata hivyo, Hailemariam aliongeza kuwa ataendelea kushikilia wadhifa huo kwa muda mpaka waraka wake wa kujiuzulu utakapokubaliwa na chama tawala nchini humo, EPRDF, na bunge la taifa hilo.


Bunge la nchi huyo linatarajiwa kukutana siku ya Ijumaa kumchagua mrithi wa Hailemariam na inatarajiwa kuwa waziri wa mambo ya nje wa nchi hiyo,  Workneh Gebeyehu, atachaguliwa kuchukua nafasi hiyo.



Mamia ya watu wamepoteza maisha katika wimbi la ghasia nchini kote ambazo awali zilichochewa na mpango wa maendelea ya mji mkuu, Addis Ababa, mwaka  2015.


Ghasia zilisambaa baada ya maandamano dhidi ya uminywaji wa uhuru wa kisiasa na ukiukwaji wa haki za binadamu yalipoibuka.


WAFUNGWA WAACHIWA HURU


Maandamano ya kudai uhuru zaidi yalianza mwaka 2015 na kuenea sana katika mikoa ya Oromia na Amhara, ambayo ni maeneo yenye wakazi wengi zaidi, kabla ya kusambaa kwenye maeneo mengine ya nchi hiyo.


Ghasia hizo zilipelekea kutangazwa kwa hali ya dharura iliyodumu kwa miezi kadhaa.


Kwa muda mrefu serikali imekuwa ikituhumiwa kuwakamata waandishi wa habari wanaoikosoa serikali na viongozi wa upinzani.


Mashirika ya haki za binadamu na makundi ya upinzani yamekuwa yakitoa wito wa kuachiwa huru kwa wakosoaji hao, yakisema kuwa wamekamatwa kwa tuhuma za kutungwa na kwamba wanaadhibiwa kwa sababu ya maoni yao.


Mnamo mwezi Januari, Hailemariam alitangaza kuwa serikali yake ingewaachia huru wafungwa hao na mpaka sasa wafungwa wapatao 7,000 wameondolewa mashitaka au kusamehewa.


Kiongozi huyo mwanataaluma aliyegeukia siasa ameiongoza Ethiopia tangu mwaka 2012, baada ya kifo cha kiongozi wa zamani Meles Zenawi.



Wakati wa utawala wa Meles alihudumu kama naibu waziri mkuu na waziri wa mambo ya kigeni kabla ya wadhifa huo, na pia alichaguliwa kuwa mwenyekiti wa Umoja wa Afrika mwaka 2013.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment