MORGAN TSVANGIRAI AFARIKI DUNIA


Tsvangirari revealed in 2003 he was being treated for colon cancer [File: Marcel Mettelsiefen/Getty Images]

Kiongozi wa upinzani nchini Zimbabwe, Morgan Tsvangirai, amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 65 kutokana na saratani, maafisa wa chama chake wamesema.


Makamu wa rais wa chama cha Movement for Democratic Change (MDC), Elias Mudzuri, alitoa taarifa ya kifo cha Tsvangirai kupitia mtandao wa Twitter mapema Jumatano usiku.


"Ninasikitika kutangaza kwamba tumempoteza kinara wetu na mpiganiaji wa demokrasia," aliandika Mudzuri.


Tsvangirai alikuwa akienda mara kwa mara katika hospitali nchini Afrika Kusini baada ya kundulika kuwa na maradhi ya saratani ya matumbo mwaka 2016.


Aliwahi kuwa waziri mkuu chini Rais wa zamani wa nchi hiyo Robert Mugabe katika serikali ya umoja wa kitaifa iliyoundwa mwaka 2009 mpaka 2013.


Naye msemaji wa chama chake, Obert Gutu, alithibitisha taarifa za kifo cha Tsvangirai kupitia mtandao wa Twitter, akimuelezea kama "kinara wa kisiasa, mtu mnyenyekevu na mpambanaji asiyechoka aliyepigania taifa lenye amani, uthabiti, demokrasia na maendeleo nchini Zimbambwe".


Wiki iliyopita, Tsvangirai aliingia kwenye mtandao wa Twitter na kuelezea kuwa maradhi yake yalikuwa katika hatua za mwisho.


"Nina saratani na sijisikii vizuri sana, lakini niko thabiti na maradhi yanadhibitiwa… ninapona,” aliandika mapema Februari 6.


Wananchi katika mji mkuu wa Zimbabwe, Harare, wameshitushwa na taarifa za kifo chake, huku wakisema kuwa watamkumbuka sana.


MORGAN TSVANGIRAI NI NANI?


Alikuwa mzungumzaji mahiri. Alizaliwa mwaka 1952 katika eneo la Buhera, kusini mashariki mwa Zimbabwe. Baba yake alikuwa fundi ujenzi.


Zimbabwe ilipopata uhuru wake kutoka kwa Muingereza mwaka 1980, Tsvangirai alichaguliwa kuwa mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi Migodini, akipanda ngazi mbalimbali mpaka kuwa katibu mkuu wa Baraza la Vyama vya Wafanyabiashara nchini humo (ZCTU) mwaka 1988, nafasi ambayo aliachana nayo baada ya kuunda chama chake cha kisiasa cha Movement for Democratic Change (MDC) mwaka 1999.


Katika uchaguzi wa mwaka 2008 alikuwa mshindani mkuu wa Mugabe na chama chake cha ZANU-PF. Alifanikiwa kupata asilimia 47 ya kura dhidi ya asilimia 43 za Mugabe, lakini kura hizo hazikumuwezesha kutawazwa kuwa mshindi wa moja kwa moja, na hivyo uchaguzi wa marudio ulitangazwa.


Tsvangirai aligomea uchaguzi wa marudio, akielezea vitisho na unyanyasaji dhidi ya wafuasi wake, na hivyo kumfanya Mugabe kuwa mshindi.


Viongozi wa kanda na wale wa jumuiya ya kimataifa waliingilia kati, na baada ya miezi kadhaa ya mazungumzo Tsvangirai aliapishwa kama waziri mkuu mwaka 2009. Ilikuwa serikali ya muda ya kugawana madaraka, lakini Mugabe aliendelea kuwa rais.


Katika uchaguzi wa urais wa mwaka 2013, chama cha Tsvangirai kilishindwa vibaya. Wakosoaji wake walisema kuwa alikuwa amesahau shida za masikini na kutamalakiwa na ulevi wa mali na madaraka.


Kifo cha Tsvangirai kimetokea ikiwa ni miezi michache kabala ya Wazimbabwe kuelekea kwenye vituo vya kupigia kura kumchagua rais mpya kufuatia kujiuzulu kwa Mugabe, ambaye amerithiwa na Emmerson Mnangagwa.


Wachambuzi wa siasa za Zimbabwe wanasema kuwa kifo cha Tsvangirai ni pigo kubwa kwa upinzani nchini humo.


Wanasema kuwa kumpata mtu mpya na kujaribu kujenga jina lake nchini ndani ya kipindi cha miezi minne ni kazi ngumu sana.



Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment