![]() |
| Motiur Rahman Nizami, kiongozi aliyenyongwa wa chama cha Jamaat-e-Islami cha nchini Bangladesh |
Serikali ya Bangladesh imemnyonga kiongozi wa chama cha Jamaat-e-Islami
kwa jinai zilizofanywa wakati nchi hiyo ikipigania uhuru wake dhidi ya Pakistan
mwaka 1971.
Kwa mujibu wa Waziri wa Sheria na Haki nchini humo Anisul
Huq, kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 73, Motiur Rahman Nizami alinyongwa jana
alfajiri katika jela moja katika mji mkuu Dhaka ikiwa ni wiki moja baada ya
kupoteza rufani yake ya mwisho katika juhudi zake za kutengua hukumu hiyo ya
kifo.
Mnamo Mei 5, Mahakama Kuu nchini humo ilitupilia mbali
rufani ya mwisho ya Nizami kupinga humu ya kifo iliyotolewa dhidi yake Januari
6. Mapema Oktoba 2014, Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ilimkuta na gatia ya
mauaji, ubakaji na kuchochea mauaji ya wasomi wakubwa wakati wa vita vya
kupigania uhuru wa taifa hilo wa kujitenga na iliyokuwa ikijulikana kama
Pakistan ya Mashariki mwaka 1971.
Nizami alikataa kuomba msamaha wa Rais Abdul Hamid. Pia shirika
la Amnesty International lilitoa wito wa kusitisha mara moja hukumu hiyo.
Nizami ni kiongozi wa nne katika viongozi wakubwa wa
chama hicho kunyongwa tangu Waziri Mkuu wa Bangladesh, Sheikh Hasina alipounda
mahakama ya kushughulikia uhalifu wa kivita mwaka 2009.
Kwa mujibu wa waendesha mashitaka, Nizami alihusika na
uanzishaji wa kundi la wanamgambo la al-Badr lililokuwa likiisaidia Pakistan
mwaka 1971, ambalo lilidaiwa kutekeleza mauaji ya wasomi wakubwa kama vile
waandishi, madaktari na waandishi wa habari katika vita ambavyo, kwa mujibu wa
takwimu za serikali, viliua watu wapatao milioni tatu.
![]() |
| Askari wa Bangladesh wakiwa wameimarisha ulinzi nje ya gareza mjini Dhaka Meo 10, 2016 ambapo kiongozi wa chama cha Jamaat-e-Islami Motiur Rahman Nizami alipangwa kunyongwa. |
Hata hivyo, Chama cha Jamaat-e-Islami, kilikanusha
vikali mashitaka hayo na kuyataja kuwa mashitaka ya uongo yenye makusudi ya
kuuondosha uongozi wa chama.
“Nizami amenyimwa haki. Ni mhanga wa kisasi cha kisiasa,”
alisema Maqbul Ahmad ambaye anakaimu uongozi wa chama.
Wakati huo huo, vikosi vya usalama viko katika tahadhari
kubwa katika maeneo yote ya nchi hiyo kufuatia hofu ya maandamano kupinga hatua
ya kunyongwa kwa Nizami.
Nizami alichukua uongozi wa chama mwaka 2000. Pia aliwahi
kuwa waziri wa kilimo kuanzia mwaka 2001 mpaka 2003, na waziri wa viwanda
kuanzia mwaka 2003 mpaka 2006.
Mnamo Agosti 2013, Mahakama Kuu ilitoa hukumu ya kufuta
usajili wa chama cha Jamaat-e-Islami na kukizuia kushiriki chaguzi za kitaifa. Viongozi
wa chama hicho wanatuhumiwa na serikali ya Bangladesh kuwa waliiunga mkono
Pakistan katika vita vya kupigania uhuru.
Kupata habari kupitia WhatsApp: +255 712 566 595
Kupata habari kupitia WhatsApp: +255 712 566 595


0 comments:
Post a Comment