KOREA KUSINI YAITUHUMU KASKAZINI KURUSHA KOMBORA JIPYA

In this undated photo, North Korean leader Kim Jong-un watches a ballistic rocket launch drill  at an unknown location, March 11, 2016. (Via Reuters)
Katika picha hii, kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un akishuhudia mazoezi ya kurusha kombora la masafa marefu katika eneo lisilojulikana, Machi 11, 2016 (Reuters)



Korea ya Kusini imesema kuwa Korea ya Kaskazini inaonekana kuwa imerusha kombora jingine baharini kwenye pwani yake ya mashariki wakati ambapo mivutano inaendelea kwenye Peninsula hiyo ya Korea.

Wizara ya Ulinzi ya Korea ya Kusini imesema kuwa kombora hilo linaonekana kutupwa leo kutokea mji wa Sondok.

Umbali na mtupo wa kombora hilo haivikuweza kuthibitishwa mara moja, kwa mujibu wa afisa mmoja wa wizara hiyo.

Wakati huo huo, shirika la habari la Korea ya Kusini, Yonhap, limesema kuwa kombora hilo linaonekana kuwa la masafa marefu.


‘Muungano’ dhidi ya Kaskazini


Tukio hilo linatokea katika kipindi ambacho Rais wa Marekani Barack Obama akiwa ameitisha mkutano wa dunia juu ya usalama wa nyuklia mjini Washington.
Pembezoni mwa mkutano huo, Obama ameungana na mwenzake wa Korea Kusini Park Geun-hye, na Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe, na kuahidi kuongeza shinikizo dhidi ya Pyongyang kama jibu dhidi ya majaribio yake ya nyuklia na makombora.

Rais Barack Obama (katikati) katika mkutano wa pande tatu pamoja na mwenzake wa Korea Kusini, Park Geun -hye (kushoto), na Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe kwenye kilele cha mkutano wa usalama wa nyuklia mjini Washington, Machi 31, 2016.


“Tumeungana katika juhudi zetu za kuzuia na kujilinda dhidi ya uchokozi wa Korea Kaskazini,” Obama aliwaambia wanahabari kufuatia mkutano huo wa pande tatu, ambao ulisisitiza haja ya jumuiya ya kimataifa kuchukua hatua dhidi ya Pyongyang.

Mwezi uliopita, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lenye wanachama 15 lilipitisha vikwazo vikali kabisa dhidi ya Korea Kaskazini. Vikwazo hivyo vilipendekezwa na Marekani.


Suluhisho la Kidiplomasia kwa suala la Korea


Wakati hayo yakitokea, wakati wa mkutano huo, Rais wa China Xi Jinping ametoa wito wa kufanyika mazungumzo kwa lengo la kutatua tatizo la Peninsula ya Korea.

“China iko tayari kufanya juhudi katika namna bora kuanzisha mazungumzo yatakayozishirikisha pande sita,” shirika la habari la China, Xinhua lilimnukuu Rais Xi akisema hapo jana wakati alipokutana na mwenzake wa Korea ya Kusini mjini Washington.

Rais wa China, Xi Jingping akizungumza wakati wa mkutano na mwenzake wa Marekani, Barack Obama kwenye kilele cha mkutano wa usalama wa nyuklia mjini Washington, Machi 31, 2016.

Mazungumzo ya pande sita aliyoyakusudia yanazihusisha Urusi, China, Marekani, Japan, Korea ya Kusini na Korea ya Kaskazini. Mazungumzo hayo yalikwama mwaka 2009 baada ya Umoja wa Mataifa kuiwekea Pyongyang vikwazo vizito kwa kufanya majaribio ya silaha za nyuklia na makombora.

Wakati huo huo, vyombo vya habari vya Korea ya Kaskazini viliuita mkutano huo wa masuala ya nyuklia kuwa ni wa “kipuuzi” kwa kuwa unajaribu kukosoa kitu ambacho Korea ya Kaskazini inakiona kuwa ni “uhalali wake wa kutumia silaha za nyuklia”.

Katika hatua nyingine, Muungano wa Ulaya umeongeza muda wa vikwazo vya kibiashara na kifedha dhidi ya Korea Kaskazini.


Muungano huo wenye wanachama 28 umesema kuwa hatua hizo mpya zimewekwa dhidi ya usafirishaji na uingizaji wa bidhaa zinazoweza kuongeza uwezo wa vikosi vya jeshi la nchi hiyo.

Aidha, Muungano huo umeongeza vikwazo dhidi ya Korea ya Kaskazini, ikiwa ni pamoja na kuzishikilia mali za serikali zenye uhusiano na programu za nyuklia au makombora ya masafa marefu ya nchi hiyo.

Mivutano kati ya Korea hizo mbili imeongezeka tangu mwanzoni mwa mwaka 2015 baada ya Kaskazini kufanya jaribio la nyuklia mwezi januari na uzinduzi wa kombora la masafa marefu ililolifanya mwezi Februari.

Pyongyang ilisema kuwa urushaji wa kombora hilo ulilenga kuweka satelaiti ya uchunguzi wa ardhi angani. Hata hivyo, Washington na Seoul zilikosoa hatua hiyo na kusema kuwa ililenga kuficha ukweli kwamba ni jaribio la kombora la masafa marefu.

Korea Kaskazini imeahidi kujenga ghala la nyuklia katika juhudi za kujilinda dhidi ya jeshi la Marekani, ambalo mara kwa mara hutuma meli za kivita zenye silaha za nyuklia na ndege zenye uwezo wa kubeba silaha za atomiki kwenye eneo hilo.

Washington pia hufanya mazoezi ya kijeshi pamoja na Korea Kusini, ambayo Korea ya Kaskazini inayaona kuwa ni maandalizi ya vita na ni kitisho cha moja kwa moja dhidi ya usalama wake.

(WhatsApp: +255 763 348 213)


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment