UKAWA KUVUNJIKA? ALIYEKUWA NAIBU KATIBU MKUU CUF KAANDIKA MTAZAMO WAKE

UKAWA kuvunjika? aliyekuwa Naibu katibu mkuu CUF kaandika mtazamo wake. 

Tangu juzi kumekuwapo na tetesi kuwa vyama vinavyounda umoja wa katiba ya wananchi UKAWA, huenda umoja huu ukasambaratika kwa kile kinachoelezwa kutokukubaliana kwa mgawanyo sawa wa majimbo kuelekea uchaguzi mkuu Oktoba.

Imeripotiwa pia leo vijana wa chama cha wananchi CUF na NCCR mageuzi, wanatarajia kuandamana ili kushinikiza viongozi wa juu wa vyama vyao kuachana na UKAWA kwa kile wanachokiita kupunjwa usawa wa uwakilishi katika majimbo na CHADEMA.

Aliyekuwa Naibu katibu mkuu wa CUF Tanzania bara, Julius Mtatiro amekuwa akitoa mtazamo wake mara kwa mara kuhusu kadhia na migogoro hii ya UKAWA, akisisitiza kutokukubaliana na kuvunjika kwao.

Kwenye ukurasa wake wa Facebook ameandika yafuatayo:

“SHEREHE ZA KUVUNJA UKAWA??? Ndugu zangu, Tangu jana nimeona MATAMKO ya watu mbalimbali wakijinasibu kwamba ni bora UKAWA ivunjike, wengine wanasema vyama vyao vinamezwa, wengine wanasema hawakubali hili na lile n.k. bahati mbaya haya yasemwayo ni mambo ambayo viongozi wa juu wa UKAWA ndiyo wanapaswa kuyashughulikia, si viongozi wa kawaida wa vyama au wanachama.

Mimi nataka tena kurudia kusema hapa, kwamba UKAWA ikivunjika kwa sababu yoyote ile, ni KITENDO CHA VYAMA VYA UPINZANI KUWASALITI WANANCHI. Hakuna lugha nyingine.
Na wale wanaofurahia UKAWA ikitetereka na wanaoombea ivunjike waendelee kuomba maombi hayo yasiyo na tija kwa taifa. UKAWA ikishavunjika vyama vya upinzani havitabaki salama hata kidogo.

Athari ambazo chama kimojakimoja kinazipata ndani ya UKAWA ni chache kuliko chama kimojakimoja kikienda kivyake. UKAWA ilikuwa na malengo makubwa sana, achilia mbali uchaguzi, kuna ajenda ya katiba.

Tuliondoka kwenye bunge la katiba na kuacha milioni 30 kila mjumbe kwa sababu ya kujenga mshikamano wa upinzani. Kuvunja UKAWA leo ni kusema pia TUNAIKUBALI KATIBA inayopendekezwa. Tukivunja UKAWA leo tunapigwa kwenye uchaguzi mkuu huu uu lakini zaidi ya yote wananchi watatupiga mawe tutakapojipeleka kuwaambia waikatae Katiba inayopendekezwa kwani tutakuwa hatuaminiki kwa mambo madogo na hatuwezi kuaminika kwa mambo makubwa.

Mimi naamini katika USHIRIKIANO WA VYAMA VYA KIMABADILIKO ili kulikomboa taifa, siamini kinyume chake hata kidogo. Kwa sababu viongozi waliahidi leo ndipo wataamua mustakabali wa kila kitu, kila mpenda mabadiliko anasubiri kwa hamu kujua viongozi wanaongoza tupite njia ipi. Mungu awabariki nyote,” ameandika Mtatiro.
Tafadhali tuachie maoni yako hapo chini, na endelea kukaa karibu na mzizima24.com

CHANZO: TIMES FM



Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment