KURA ZA MAONI CHADEMA LAWAMA, UBABE VYATAWALA

Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Wilbroad Slaa.


Wakati mchakato wa kuwatafuta wagombea watakaosimama kupeperusha bendera ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ngazi ya ubunge ukiendelea katika sehemu mbalimbali nchini, zimejitokeza dosari huku maeneo mengine mikutano ikivunjika.

MTWARA

Wanachama wa Chadema wilaya ya Mtwara wameshindwa kupata wagombea ubunge katika jimbo la Mtwara Mjini na wa Viti Maalum kutokana na kuvurugika kwa mkutano kufuatia mkanganyiko juu ya idadi ya kata zilizofanya uchaguzi na kuwa na uhalali wa kupiga kura za kuchagua wagombea.

Wagombea waliokuwa wanachuana ni Joel Nanauka, Mohamed Hassan Hanga, Ibrahim Mandoa na Dastani Mulokozi ambaye hakuwapo mkutanoni na kuwakilishwa na mke wake.

Hatua hiyo ilitokana na hoja iliyotolewa na mjumbe wa mkutano huo ambaye ni mwenyekiti wa mawasiliano, takwimu na Biometric Voters Registration (BVR), Karim Salum Ally, ambaye alihoji utofauti wa idadi ya kata hizo kwamba taarifa alizokuwanazo yeye ni kata 15 huku zile za katibu wa Chadema mkoa, Willy Mkapa zilisema ni kata 17.

BARIADI

Katika jimbo la Bariadi, zilitokea dosari baada ya mkutano wa kumpata mgombea wa nafasi hiyo kuvunjika.

Mkutano huo ulivunjika saa 9:30 alasiri, baada ya viongozi wa chama hicho wilaya na wasimamizi kubaini kuwapo kwa vitendo vya rushwa kwa wagombea kubainika kugawa fedha kwa baadhi ya wajumbe ili wawapigie kura.

Kabla ya kuvunjika kwa mkutano huo saa 6:00 mchana, baadhi ya wapambe wa wagombea wakiwa wanagawa pesa hadharani kwa wajumbe, vijana wa ulinzi wa chama hicho (red briged), waliwakamata wanawake wawili na kijana mmoja wa wapambe hao.

Hata hivyo, baada ya kiongozi wa vijana wa ulinzi wa Chadema wa kanda ya Serengeti, Esau Bwire, alisema watu hao walibainika wakigawa Sh. 20,000 kwa kila mjumbe.

Msimamizi wa uchaguzi huo wa kanda ya Serengeti, Emmanuel Mbise, alithibitisha kuwapo kwa vitendo vya rushwa kwa wagombea kadhaa na kukichafua chama wakati kikipiga vita vitendo hivyo.

Licha ya kuwapo wagombea 12 wa nafasi ya ubunge katika jimbo hilo, lakini alishindwa kupatikana mmoja kati yao kutokana na kuvunjika kwa mkutano huo.

SHINYANGA

Msimamizi wa uchaguzi katika jimbo la Shinyanga Mjini, Alex Malima, alimtangaza mwenyekiti wa taifa vijana Chadema (Bavicha), Patrobas Katambi, kuwania ubunge katika jimbo hilo.

Aidha, Malima alimtangaza mbunge wa viti maalumu aliyemaliza muda wake, Rachel Mashishanga, kutetea tena kiti hicho kupitia Chadema.

Mwenyekiti wa Kanda ya Ziwa Mashariki, Silvester Kasulumbai, alisema chama hicho kinachopendwa na wananchi kinatakiwa kupata watu makini watakaoweza kupeperusha  bendera ya chama katika uchaguzi ujao wa Oktoba mwaka huu.

BUSEGA

Dk. David Nicas, mgombea wa nafasi ya ubunge katika jimbo la Busega kwa tiketi ya Chadema, alifanikiwa kupata kura 116 dhidi ya washindani wake wa karibu 11 ambao ni Mabelele Buluba kura 67 na Revocatus Madundo (55).

ILEMELA

Mbunge aliyemaliza muda wake katika jimbo la Ilemela, Highness Kiwia, aliibuka mshindi kwa kupata kura 134 kati ya kura 294 zilizopigwa kwa wagombea wenzake 18.



CHANZO: NIPASHE
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment