MTEKAJI WA NDEGE ATIWA NGUVUNI MJINI ISTANBUL





Vikosi vya usalama nchini Uturuki vimefanikiwa kumtia nguvuni abiria alijaribu kuiteka ndege iliyolazimishwa kutua mjini Istanbul usiku wa leo.

Afisa mmoja kutoka wizara ya uchukuzi nchini humo amekaririwa akisema kuwa wakati wa zoezi hilo hakuna maafa yaliyotokea na kwamba abiria wote wameondolewa katika ndege.

Ndege hiyo iliyokuwa na abiria 110 kutoka Ukraine ililazimishwa na ndege za jeshi la Uturuki kutua katika uwanja wa ndege wa Sabiha Gokcen mjini Istanbul baada ya kuwepo kwa jaribio la utekaji ambapo mtekaji huyo alitangaza kuwepo kwa bomu ndani ya ndege  na kutaka ielekezwe mjini Sochi nchini Urusi ambapo michezo ya Olimpiki ya Majira ya Baridi inaendelea.

Itakumbukwa kuwa Januari 20 mwaka huu, kundi moja la wanamgambo Kaskazini mwa Urusi lilitishia kufanya mashambulizi dhidi ya michezo hiyo ya Olimpiki.

Katika mkanda wa video uliorushwa mtandaoni, kundi hilo lilimuonya Rais wa Urusi Vladimir Putin asikaribishe michezo hiyo, likisema kuwa wale watakokwenda Sochi wangepokelewa kwa “matukio ya kushtukiza.”

Wanamgambo hao waliojitokeza katika video hiyo, walidai pia kuhusika na mashambulizi pacha ya mabomu katika kituo kimoja cha treni na katika basi moja la abiria katika mji wa kusini wa Volgograd mwezi Desemba, ambapo watu zaidi ya 30 walipoteza maisha.

Hata hivyo, Rais Putin aliahidi kuhakikisha amani na usalama wakati wa michezo hiyo inayofanyika katika mji huo ulio kandokando mwa pwani ya Bahari Nyeusi.

“Kama waandaaji wa wa mashindano haya, tunawajibika kutoa dhamana ya usalama wa wanamichezo na wageni wa michezo hii ya Olimpiki na tutafanya kila liwezekanalo kufikia lengo hili,” alisema Putin alipotembelea mji huo wa Sochi mwezi jana.

Putin alifanya ziara mjini Sochi siku moja baada ya kufanya mkutano na mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao mjini Moscow ambapo aliwaambia kuwa mashindano hayo yangefanyika bila ubaguzi wowote dhidi ya wanamichezo na wageni.

Michezo ya Olimpiki Majira ya Baridi imeanza rasmi Februari 7 mpaka 23, na kwa mara ya kwanza katika historia ya michezo hiyo, wageni wataweza kusafiri kwenye mji mwenyeji bila visa.


Hata hivyo, vitisho dhidi ya mashindano hayo vimeongezeka licha ya hakikisho hilo lililotolewa na Rais Putin.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment