VIONGOZI WA DUNIA WAOMBOLEZA KIFO CHA MANDELA






Rais Jakaya Mrisho Kikwete ameungana na viongozi mbalimbali dunia kuomboleza kifo cha shujaa wa mapambano ya siasa za ubaguzi wa rangi na rais wa zamani wa Afrika Kusini, mzee Nelson Mandela aliyefariki jana usiku.

Katika salamu zake za rambirambi kwa rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma na Mke wa Mandela Bi.Graca Machel rais Jakaya Kikwete amemtumia Salamu za rambirambi Rais Jacob Zuma wa Afrika ya Kusini na kupitia kwake, kwa mkewe Bi. Graca Machel, rais Kikwete amesema msiba huu kuwa ni msiba mkubwa kwa Afrika ya Kusini, Afrika na dunia kwa ujumla imepoteza mtu mashuhuri na shujaa mkubwa wa Karne ya 20 na 21.
Amesema Afrika Kusini imempoteza kiongozi shupavu, jasiri, mwana mapinduzi , mvumilivu na mstahimilivu.

Amesema Mzee Mandela kuwa ni kielelezo cha aina yake kwa wanadamu kwa moyo wake wa kusamehe, huruma na upendo uliomuwezesha kuwaunganisha wananchi wa Afrika ya Kusini kuwa taifa moja baada ya kipindi kirefu cha mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi. .

Aidha, Rais Kikwete ametangaza maombolez ya siku 3 kuanzia leo hadi Desemba 8 kufuatia kifo cha aliyekuwa rais wa kwanza mzalendo wa Afrika Kusini Mzee Nelson Mandela.


Sambamba na hilo bendera itapepea nusu mlingoti ka siku zote tatu za maombolezo.

Usiku wa jana, Rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma alitangaza kifo cha mzee Mandela akisema kuwa taifa hilo limempoteza mmoja wanataifa wakubwa kabisa.

"Mapambano yake ya kupigania uhuru bila kuchoka yalimpatia heshima kubwa ulimwenguni. Unyenyekevu wake, huruma yake na utu wake viliwafanya watu wampende,” alisema Zuma.

RAIS OBAMA

Rais wa Marekani, Barack Obama alielezea huzuni yake kuhusu kifo cha Mandela, na kumuelezea kuwa alikuwa “mtu mwenye nguvu, jasiri na mwenye ushawishi ambaye kila mtu angependa kuishi naye, na kwamba alipata mafanikio ambayo kila mtu angetamani kuyapata. Leo amerejea nyumbani.”

Obama alionegeza kuwa, “sas sio mtu wetu tena; ameondoka.”

CLINTON

Rais mstaafu wa Marekani ameungana na viongozi wengine kuomboleza kifo cha Mandela na kumuelezea kama “shujaa wa utu na uhuru wa mwanadamu.”

"Leo dunia imempoteza mmoja wa viongozi wake muhimu kabisa na mmoja wa watu wazuri kabisa,” alisema Clinton.

"Historia itamkumbuka Nelson Mandela kama shujaa wa utu na uhuru wa binadamu, shujaa wa amani na maridhiano. Tutamkumbuka kama mtu aliyekuwa na huruma isiyokuwa ya kawaida, aambaye kuukabili uchungu na changamoto mbalimbali haikuwa tu mbinu yake ya kisiasa bali ilikuwa mfumo wa maisha yake,” aliongeza.

RAIS WA BRAZIL

Naye Rais wa Brazil, Dilma Rousseff, amemuelezea Mandela kama mfano kwa wale wanaopigania haki na amani. “Mfano wa kiongozi huyu mkubwa utakuwa muongozo kwa wale wote wenye kupigania haki ya kijamii na amani duniani.” Alisema Rais Dilma.

IRAN

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Mohammad Jawad Zarif aliandika katika ukurasa wake wa twitter:  

“Wairan tunaungana na wananchi wa Afrika Kusini kuomboleza kifo cha Nelson Mandela ambaye amewahamasisha wanadamu kwa ujasiri na huruma,” alisema Zarif.

UFARANSA

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa, Laurent Fabius, ametoa salamu zake za rambirambi kwa Mandela, akimuelezea kuwa "mtu aliyekuwa na karisma.”

"Kwa kifo cha Nelson Mandela, baba wa Afrika Kusini, nguvu ya uhuru na maridhiano imekufa,” alisema Fabius.

UINGEREZA

Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron amesema kuwa “nuru adhimu imezimika ulimwenguni. Nelson Mandela alikuwa mtu mtu adhimu katika zama zetu; shujaa katika uhai na sasa shujaa katika mauti—shujaa wa kweli wa dunia.”

AUSTRALIA

Naye Waziri Mkuu wa Australia, Tony Abbott, amemsifu Mandela kama “shujaa wa kweli,” akisema kuwa, "Nelson Mandela miongoni mwa viongozi wakubwa kabisa wa bara la Afrika, na kwa kweli alikuwa mmoja wa viongozi wakubwa kabisa wa karne iliyopita.”

"Wakati dunia inaweza isimuone tena Nelson Mandela mwengine, amekuwa hamasa ya wanaume na wanawake wengi duniani kote aliyewafanya waishi maisha ya ujasiri na uaminifu,” aliongeza Abbott.

UJERUMANI

Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel amesema, "mfano angavu wa Nelson Mandela na athari yake ya kisiasa ya kutotumia vurugu na kuzilaani aina zote za ubaguzi wa rangi vitaendelea kuwapa hamasa watu ulimwenguni kote kwa miaka mingi ijayo.”

MEXICO
Rais wa Mexico Enrique Pena Nieto amesema kuwa, "binadamu wamempoteza shujaa asiyechoka kupigania amani, uhuru na usawa.”

ASKOFU DESMOND TUTU

Naye askofu Desmond Tutu ameomboleza kifo cha Mandela, akimuelezea kama “mfano wa utangamano, mfano wa maridhiano, mfano wa uongozi katika kuwahudumia watu.”

"Kwa hakika, alikuwa mtu wa aina yake, lakini moyo wa ukuu aliokuwa nao unaishi pamoja nasi sote,” aliongeza.

UMOJA WA MATAIFA

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon amesema, “ni kwa sababu tu ya mtu adhimu kama Nelson Mandela imewezekana kwa watu Afrika na kwengineko kufurahia uhuru na heshima ya utu. Tunapaswa kujifunza hekima, azma na uwajibikaji wa Mandela ili kuifanya dunia kuwa sehemu bora kwa ajili ya watu wote.”

Mandela, ambaye aliongoza mapambano dhidi ya utawala wa weupe wachache katika miaka ya 1990 baada ya kukaa karibu miongo mitatu gerezani, alikuwa miongoni mwa wanasiasa wakubwa kabisa wa karne ya 20.


Baada ya miaka kadhaa ya harakati za mapambano dhidi ya utawala wa kibaguzi wa Afrika Kusini, Mandela alikamatwa mwaka 1962. Alihukumiwa adhabu ya kifungo cha maisha gerezani, ambapo alitumikia miaka 27 tu, ambayo sehemu kubwa aliitumikia katika gereza katika Kisiwa cha Robben nchini humo.

Baada ya kuachiwa huru kutoka gerezani Februari 11, 1990, Mandela alikiongoza chama cha African National Congress (ANC) katika mazungumzo yaliyopelekea kufanyika kwa uchaguzi wa kidemkrasia uliowajumuisha watu wote ambao ulifanyika mwaka 1994. Akiwa kama rais, kipaumbele chake kikubwa alikiweka katika utangamano na maridhiano. Alistaafu mwaka 1999 baada ya kutumikia kipindi kimoja tu cha urais.

Nchini Afrika Kusini, Mzee Mandela anajulikana sana kwa jina la ukoo la Madiba, au tata, yaani baba.

Mandela amepokea zaidi ya tuzo 250 ndani ya miongo minne, ikiwemo Tuzo ya Amani ya Nobel aliyoipata mwaka 1993.

Mwaka 2004, mzee Mandela alitangaza kuacha kujihusisha na shughuli za umma lakini akaendelea kuonekana katika matukio machache sana.

Endelea kufuatilia hapa hapa Mzizima 24..


www.mzizima24.com
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment