MZEE MANDELA AMEFARIKI DUNIA

South Africa



Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini usiku huu ametangaza kuwa shujaa wa mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi na rais mstaafu wa nchi hiyo, Mzee Nelson Mandela amefariki dunia.

Katika taarifa yake yenye huzuni katika televisheni ya taifa ya nchi hiyo, Rais Zuma aliyejawa na majonzi ametangaza kuwa mzee Mandela “amefariki kwa amani.” Amesema kuwa taifa lake limempoteza mmoja wazalendo wake wakubwa kabisa.

Mandela, ambaye aliongoza mapambano dhidi ya utawala wa weupe wachache katika miaka ya 1990 baada ya kukaa karibu miongo mitatu gerezani, alikuwa miongoni mwa wanasiasa wakubwa kabisa wa karne ya 20.

"Wananchi wamempoteza baba. Ingawa tulijua kwamba siku hii itafika, hakuna kinachoweza kuiondosha msiba huu mkubwa tulioupata,” alisema Zuma.

"Mapambano yake ya kupigania uhuru bila kuchoka yalimpatia heshima kubwa ulimwenguni. Unyenyekevu wake, huruma yake na utu wake viliwafanya watu wampende. Fikra na sala zetu ziko pamoja na familia ya Mandela. Hakika tuna deni la kuwashukuru. Fikra zetu ziko pamoja na mkewe, mkewe wa zamani, watoto wake, wajukuu wake, vitukuu na familia yote,” aliongeza.

Mandela alikuwa akipatiwa matibabu nyumbani kwake kutokana na maambukizi katika mapafu yake baada ya kukaa hospitali kwa muda wa miezi mitatu. Alikuwa akisumbuliwa na tatizo la upumuaji, ambalo yamkini lilitokana na taathira aliyoipata wakati akiwa gerezani.

"Fikra zetu ziko pamoja na mamilioni ya watu ulimwenguni kote ambao walimchukulia Nelson Mandela kama sehemu ya maisha yao na ambao waliyaona mapambano yake kama mapambano yao. Hiki ni kipindi cha msiba mkubwa kabisa,” alisema Rais Zuma katika taarifa yake.

"Ni wazi kuwa kilichomfanya Nelson Mandela kuwa mtu mkubwa ni kile kilichomfanya kuwa na utu. Ndani mwake tunaziona sifa ambazo tungependa kuwa nazo,” alisema Zuma.

Mandela alikuwa rais wa Afrika ya Kusini kuanzia mwaka 1994 mpaka 1999, na ndiye rais wa kwanza wa nchi hiyo kuchaguliwa katika uchaguzi wenye demokrasia shirikishi iliyowahusisha watu wote wa nchi hiyo.

Baada ya miaka kadhaa ya harakati za mapambano dhidi ya utawala wa kibaguzi wa Afrika Kusini, Mandela alikamatwa mwaka 1962. Alihukumiwa adhabu ya kifungo cha maisha gerezani, ambapo alitumikia miaka 27 tu, ambayo sehemu kubwa aliitumikia katika gereza katika Kisiwa cha Robben nchini humo.

Baada ya kuachiwa huru kutoka gerezani Februari 11, 1990, Mandela alikiongoza chama cha African National Congress (ANC) katika mazungumzo yaliyopelekea kufanyika kwa uchaguzi wa kidemkrasia uliowajumuisha watu wote ambao ulifanyika mwaka 1994. Akiwa kama rais, kipaumbele chake kikubwa alikiweka katika utangamano na maridhiano. Alistaafu mwaka 1999 baada ya kutumikia kipindi kimoja tu cha urais.

Nchini Afrika Kusini, Mzee Mandela anajulikana sana kwa jina la ukoo la Madiba, au tata, yaani baba.

Mandela amepokea zaidi ya tuzo 250 ndani ya miongo minne, ikiwemo Tuzo ya Amani ya Nobel aliyoipata mwaka 1993.

Mwaka 2004, mzee Mandela alitangaza kuacha kujihusisha na shughuli za umma lakini akaendelea kuonekana katika matukio machache sana.



Taarifa zaidi zitaendelea kukujia hapa hapa Mzizima 24..
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment