WAANDAMANAJI WAVAMIA MAKAO MAKUU YA JESHI



Waandamanaji mjini Bangkok, Thailand

Waandamanaji wa upinzani nchini Thailand wamefika makao makuu ya jeshi la nchi hiyo mjini Bangkok, wakitaka jeshi liyaunge mkono maandamano yao.

Waandamanaji hao wanaipinga serikali ya Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Yingluck Shinawatra, ambaye ni dada wa waziri mkuu wa zamani na bilionea wa biashara ya mawasiliano, Thaksin Shinawatra, aliyeondolewa katika mapinduzi ya mwaka 2006. Wananchi wanalalamika kuwa Thaksin bado anaiendesha serikali ya dada yake kwa namna isiyokuwa ya moja kwa moja au kwa nyuma ya mlango, na amekuwa akiishi uhamishoni tangu alipoondolewa madarakani.

Leo waandamanaji hao walilazimisha kwa nguvu kufunguliwa kwa lango la makao makuu ya jeshi na kumiminika ndani ya viwanja vya ofisi hizo.

“Tunataka kujua kama jeshi litawaunga mkono wananchi au litamuunga mkono dikteta,” alisema mmoja wa viongozi wa waandamanaji hao, Amorn Amornrattananont.

Pia waandamanaji hao walikusanyika mbele ya makao makuu ya chama cha  Puea Thai, kinachoongozwa na Waziri Mkuu, Yingluck.

Kwa siku za hivi karibuni, majengo ya serikali likiwemo jengo la wizara ya fedha mjini Bangkok yamekuwa yakizingirwa na maelfu ya waandamanaji wakiishinikiza serikali ijiuzulu.

Jana Waziri Mkuu, Yingluck Shinawatra, aliponea chupu chupu katika kura ya kutokuwa na imani naye iliyoendeshwa na bunge la nchi hiyo.


Katika taarifa yake iliyorushwa na televisheni ya nchi hiyo, Yingluck alisema kuwa serikali yake iko tayari kufungua uwanja wa majadiliano na mazungumzo, akisema kuwa maafisa wa serikali yake wapo tayari kusikiliza sauti za wananchi, wakiwemo wale waliozizingira na kuzikalia kwa nguvu ofisi za serikali.

Hata hivyo, kiongozi wa upinzani, Suthep Thaugsuban, alitupilia mbali wazo la kufanya mazungumzo.


“Yingluck anasema serikali inaweza kuendelea kutawala, inaweza kuendelea kufanya kazi – ninataka kuwaambia kuwa wataweza kufanya kazi kwa masiku kadhaa tu, baada ya hapo hatutawaacha kuendelea kufanya kazi,” Thaugsuban aliwaambia wafuasi wake mjini Bangkok.

Maandamano nchini Thailand yaliibuka baada ya bunge la seneti la nchi hiyo  Novemba 11 kuuukataa muswada unaoungwa mkono na serikali ambao ungempatia msamaha waziri mkuu wa zamani, Thaksin Shinawatra, ambaye ni kaka wa Waziri Mkuu wa sasa, na kumuwezesha kutoka uhamishono.

Thaksin Shinawatra anatuhumiwa kwa ubadhirifu, ufisadi, ufujaji wa mali ya umma pamoja na kutumia madaraka yake vibaya kiasi cha kutomheshimu mfalme wa nchi hiyo, ambaye anayetambuliwa na katiba, jambo lililosababisha kung’olewa madarakani mwaka 2006.


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment