MURSI: NILITEKWA KABLA YA KUPINDULIWA


A protester carries a poster of ousted Egyptian President Mohamed Morsi during a demonstration in central Cairo on July 15, 2013.

Na Kabuga Kanyegeri


RAIS aliyeondolewa madarakani nchini Misri, Muhammad Mursi, amesema katika barua maalumu aliyoiandika, kuwa alitekwa nwa Walinzi wa Jamhuri kabla ya jeshi kutangaza rasmi kuwa limemuuzulu mwezi Julai.

Katika barua hiyo iliyosomwa katika televisheni jana na wakili wake, Muhammad Damati, Mursi anasema: “Wananchi wema wa Misri wanapaswa kujua kuwa nilitekwa kwa nguvu na bila ridhaa yangu kuanzia Julai 2 mpaka Julai 5 katika jengo la Walinzi wa Jamhuri mpaka pale mimi na msaidizi wangu tulipohamishwa tena kwa nguvu kwenda kwenye kambi ya jeshi la maji kwa muda wa miezi minne kamili.”

Aidha, katika barua hiyo, Mursi alitangaza kuwa yeye ndiye rais halali wa Misri na kuelezea kitendo cha kuondolewa kwake madarakani kuwa ni mapinduzi ya kijeshi na ni kosa la jinai.

"Misri haitatulia mpaka yote yaliyotokea kwa sababu ya mapinduzi haya yatakapoondoka na wale waliohusika na umwagaji damu kila mahali katika taifa washitakiwe,” alinukuliwa akisema.

"Ninawapongeza wananchi wa Misri waliosimama dhidi ya mapinduzi haya, ambayo yatashindwa kwa nguvu ya umma wa Misri katika kupigania haki na uhuru wao,” aliongeza kusema.

Mapema usiku wa Julai 3, mkuu wa jeshi la Misri Jenerali Abdul Fattah al-Sisi alitangaza kuwa Mursi ameondolewa madarakani, akamtangaza mkuu wa Mahakama Kuu ya Katiba, Adly Mahmoud Mansour, kuwa rais mpya wa mpito na kusimamisha matumizi ya katiba.

Maafisa wa jeshi walisema kuwa Mursi, aliyeingia madarakani Juni 2012, alikuwa ameshikiliwa na jeshi sehemu maalumu.

Misri imekuwa katika ghasia na vurugu tangu Julai 3. Serikali ya Mansour imeanzisha operesheni maalumu dhidi ya wafuasi wa Mursi na kuwakamata zaidi ya wanachama 2,000 wa Vuguvugu la Udugu wa Kiislamu, akiwemo kiongozi mkuu, Muhammad Badie, aliyekamatwa Agosti 20.

Watu wapatao 1,000 waliuawa ndani ya wiki moja katika makabiliano baina ya wafuasi wa Mursi na vikosi vya usalama baada ya polisi kuzibomoa kambi zao katika operesheni kabambe dhidi ya wafuasi hao Agosti 14.


Mauaji hayo yaliamsha lawama za kimataifa na kuzifanya taasisi mbalimbali kutoa wito wa kufanyika kwa uchunguzi huru kuhusu ghasia na mauaji hayo.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment