MGOGORO WA KONGO: MAZUNGUMZO HAYAJAFUNGWA RASMI



Waasi wa M23 baada ya kujisalimisha kwa serikali ya Uganda


Na Kabuga Kanyegeri


Waratibu wa mazungumzo ya amani yanayofanyika mjini Kampala baina ya maafisa wa serikali ya Kongo na waasi wa M23 wamesema kuwa mazungumzo yataendelea, licha ya pande hizo mbili kushindwa kufikia muafaka hapo jana.

"Pande zote mbili bado zipo hapa Uganda… Mazungumzo hayajafungwa rasmi,” msemaji wa serikali Uganda, Ofwono Opondo, aliwaambia waandishi wa habari.

Mazungumzo yalivunjika baada ya serikali ya Kongo kutaka kuwepo kwa mabadiliko katika hati ya mkataba, licha ya kamba Waziri wa Mambo ya Nje wa Kongo, Raymond Tshibanda, alikuwa amesisitiza kuwa serikali inataka amani.

Uganda, ambayo ni mwenyeji wa mazungumzo hayo, ilisema kuwa inatarajia mazungumzo hayo yataendelea.

Mnamo Novemba 5, Kongo ilitangaza kuwa imewashinda kabisa waasi wa M23 baada ya kuziteka ngome za mwisho za kundi hilo kaskazini mwa Goma na kuhitimisha vita iliyodumu kwa muda wa miezi 20.

Saa chache baadaye, kiongozi wa M23, Bertrand Bisimwa, alitangaza kuwa kundi lake limeachana na mapigano na kwamba litaweka silaha chini na kufanya mazungumzo ya amani.

Waasi wa M23, walikuwa wakiyashikilia maeneo kadhaa mashariki mwa nchi hiyo na kuendesha mapambano dhidi ya serikali kuu.

Mapema mwaka huu, Umoja wa Mataifa uliidhinisha kupelekwa kwa kikosi maalumu kinachoundwa na wanajeshi wa Kiafrika kikiwa na mamlaka ya kupambana na waasi hao.


Licha ya kusambaratika kwa kundi la M23, ndani ya Kongo bado kuna makundi mengi ya waasi na mengi yapo katika eneo la mashariki lenye utajiri mkubwa wa madini.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment