WAFUNGWA 7 WAFARIKI DUNIA HUKO MEXICO

Relatives of inmates at a prison pull the security fence following a riot inside the detention facility in Mexico’s state of Nuevo Leon. (File photo)
Ndugu wa wafungwa wakisukumana na maafisa usalama katika jela moja ya mji wa Nuevo Leon.



KWA uchache wafungwa saba wamepoteza maisha katika jela moja katika jimbo la kasikazini mashariki la Tamaulipas nchini Mexico.

Kwa mujibu wa maafisa usalama wa jimbo hilo, ambao walizungumza kwa masharti ya kuficha majina yao, walisema kuwa tukio hilo lilitokea jana Jumamosi katika gereza moja la mji wa Altamira, kiasi cha kilomita 480 (maili 300) kusini mwa mpaka wa Mexico na Marekani.

Aidha, maafisa hao walisema kuwa wafungwa hao wenye umri kuanzia miaka 20 mpaka 50, walipoteza maisha yao katika mapigano yaliyoibuka ndani ya chumba kimoja cha wafungwa.

Maafisa wa gereza wanasema kuwa wafungwa tisa, waliokuwa na matatizo na wale waliouawa, ndio walioanza mapambano, ambapo mbali na hao waliokufa, watu wawili walijeruhiwa na wengine tisa walitiwa nguvuni.

Mwezi Januari 2012, wafungwa 31 walipoteza maisha katika ghasia zilitokea katika gereza hilo hilo, huku magereza nchini humo yakiendelea kushuhudia ghasia, vurugu, mauaji na utorokaji wa wafungwa.

Mwezi Desemba 2012, watu 17, wakiwemo askari 6, waliuawa katika ghasia zilizotokea katika gereza moja katika mji wa Gomez Palacio.

Tukio hilo lilitokea katika jimbo la Durango, wakati wafungwa walipokuwa wakijaribu kutoroka gerezani na kukimbia kupitia mifereji ya chini ya gereza hilo.

Mwezi Septemba 2012, zaidi ya wafungwa 130 nchini humo walitoroka jela iliyokaribu na mpaka wa Marekani kwa kupitia kwenye mfereji wa maji machafu wa chini ya gereza hilo.

Matukio ya wafungwa kutoroka kwa wingi kutoka magerezani yamekuwa yakiongezeka katika miaka ya hivi karibuni na maafisa wa magereza wamekuwa wakilaumiwa kwa kuwa na usuhuba na magenge yanayojihusisha na madawa ya kulevya.


Tangu mwaka 2010, matukio kadhaa ya utorokaji magerezani yamekuwa yakiripotiwa kwa wingi sana nchini Mexico. Mwezi Desemba mwaka huo, zaidi ya wafungwa 140 walitoroka katika gereza moja katika mji wa mpakani wa Nuevo Laredo katika jimbo la Tamaulipas.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment