VIKOSI VYA KONGO VYAIKAMATA NGOME YA WAASI

 Colonel Mamadou Ndala briefs North Kivu province governor Julien Paluku in Kibumba
Kamanda wa Operesheni za jeshi la Kongo katika Jimbo la Kivu Kaskazini, Kanali Mamadou Ndala, akimpa taarifa gavana wa Jimbo la Kivu Kaskazini Julieni Paluku mjini Kibumba.


VIKOSI vya serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo vimeukamata mji wa  Rutshuru katika siku ya tatu ya mapambano makali katika eneo la mashariki mwa nchi hiyo.

Mapigano hayo yalizuka siku ya Ijumaa baada ya mazungumzo ya amani baina ya serikali na waasi wa M23 kukwama baada ya waasi kutaka viongozi wao wote wasamehewe kikamilifu bila masharti yoyote.

Jana Jumapili,  msemaji wa jeshi la Kongo, Kanali Olivier Hamuli aliiambia redio ya Umoja wa Matifa, Okapi, kuwa vikosi vya serikali vimeudhibiti mji wa  Rutshuru, kiasi cha kilometa  70 (maili 43) kaskazini mwa mji wa Goma, ambao ndio mji mkubwa kabisa katika eneo la mashariki mwa Kongo.

Waasi walikuwa wakiudhibiti mji wa Rutshuru tangu mwaka mmoja uliopita. Walikuwa wakiutumia mjhuo kama ngome yao ya kijeshi ya jimbo.

Mapema Jumapili, jeshi liliukamata mji wa Kiwanja uliokuwa ukishikiliwa na waasi, siku moja baada ya mapambano makali kwenye mji muhimu wa Kibumba ambao upo kwenye mpaka wa nchi hiyo na Rwanda.

“Tunaimarisha maeneo tuliyoyachukua,” alisema Hamuli, huku akikataa kuzungumzia ombi la waasi kutaka kurudi kwenye meza ya mazungumzo: “Tutaendelea kufanya kazi zetu kama askari.”

KAULI YA M23

Katika taarifa yake ya jana Jumapiili, M23 walisema kuwa waliyaondoa majeshi yao kutoka mji wa Kiwanja na kulituhumu jeshi la Kongo kuwa liliwatuma askari wake wakiwa wamevaa nguo za kiraia ili kuwafanya askari wa Umoja wa Mataifa kuingilia kati.

Kundi hilo pia lilitishia kuwaondoa wajumbe wake kutoka katika mazungumzo yaliyokwama iwapo hakutakuwa na “usitishwaji wa haraka wa mapigano.”

ASKARI WA TANZANIA AUAWA

Wakati huo huo, tume ya Umoja wa Mataifa ya kusimamia amani ya Kongo  (MONUSCO) imesema kuwa askari mmoja wa Tanzania katika kikosi cha kulinda amani aliuawa wakati wa mapambano na waasi wa M23 katika eneo la Kiwanja.

“Askari huyo alifariki wakati akiwalinda wananchi wa Kiwanja,” alisema mkuu wa  MONUSCO, Martin Kobler, katika taarifa yake.  

Umoja wa Mataifa umetuma brigedi maalumu ya askari 3,000 wa Kiafrika wenye mamlaka ya kupambana nchini Kongo.


Makundi kadhaa yenye silaha, ikiwemo M23, wanaendesha harakati zao za uasi mashariki mwa Kongo na wanapigania kuidhibiti nchi hiyo kubwa yenye maliasili za madini, kama vile dhahabu, urani, coltan, ambayo hutumika katika utengenezaji wa vifaa vingi vya elektroniki, ikiwemo simu za mkononi.
         

Waasi wa M23 walijiondoa katika jeshi la Kongo mwezi Aprili 2012 kupinga kile walichodai kuwa ni mwenendo mbaya ndani ya jeshi la Taifa (FARDC). Walikuwa wamejumuishwa katika jeshi chini ya mkataba wa amani uliosainiwa mwaka 2009.

Tangu mwezi Mei 2012, takriban watu milioni 3 wameyekimbia makazi yao katika eneo la mashariki mwa Kongo. Takriban watu milioni 2.5 ni wakimbizi wa ndani, huku zaidi ya watu 460,000 wamekimbilia katika nchi za Rwanda na Uganda.


Kongo imekuwa ikikabiliwa na matatizo matatizo kwa miongo kadhaa, kama vile umaskini uliokithiri, miondombinu mibovu, na vita katika eneo la mashariki mwa nchi hiyo ambavyo viliibuka tangu mwaka 1998 na kugharimu maisha ya zaidi ya watu milioni 5.5.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment