UMOJA WA MATAIFA: M23 WAMEKWISHA KIJESHI



A Congolese army soldier moves forward under fire in the rebel-occupied Kasanza hill area, north of Goma, Congo, on October 25, 2013.
Askari wa Kobgo wakisonga mbele katika eneo la mlima Kasanza lililokuwa likishikiliwa na waasi, kaskazini mwa Goma, Oktoba 25, 2013.



Na Kabuga Kanyegeri


JESHI la serikali ya Kongo likisaidiwa na vikosi vya Umoja wa Mataifa limeendelea kutoa kipigo kwa waasi wa M23 waliokuwa wakitishia usalama wa miji ya eneo la mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa nchini humo amesema.

Martin Kobler, ambaye pia ni mkuu wa Tume ya Umoja wa Mataifa ya Kusimamia amani ya Kongo (MONUSCO), aliyasema hayo wakati akitoa taarifa yake kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kupitia mawasiliano ya video jana Jumatatu.

"Kwa ujumla M23 wameondoka katika maeneo yote jana, isipokuwa eneo dogo linalopatikana mpakani mwa Rwanda,” alisema.

Kobler alisema kuwa M23 waliondoka katika ngome yao muhimu kwenye Mlima Hehu jirani na mpaka wa Rwanda, akaongeza kuwa, “Kwa M23 wamefikia mwisho kijeshi.”

Gerard Araud, balozi wa Ufaransa kwenye Umoja wa Mataifa, ambaye alikuwepo wakati Kobler akitoa taarifa yake, alithibitisha ripoti hiyo.

"Leo tunaweza kusema kuwa M23 imekwisha kijeshi,” Araud aliwaambia waandishi wa habari na kusisitiza kuwa “maeneo mengi yaliyokuwa yakishikiliwa na M23 yamechukuliwa na vikosi vya jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.”

Araud na wanadiplomasia wengine kwenye Umoja wa Mataifa walielezea matarajio kuwa hatua ya waasi kushindwa kwenye uwanja wa mapambano kutawashawishi kurudi kwenye meza ya mazungumzo ya amani.

Mazungumzo ya amani kati ya serikali ya Kongo na waasi wa M23 yamesimama kutokana na kutokubaliana kwenye suala la msamaha kwa viongozi wa waasi.

Jeshi la Kongo linapambana na waasi kwa msaada wa brigedi mpya ya Umoja wa Mataifa inayoongozwa na Tanzania ikiwa na mamlaka ya kupambana. Brigedi hiyo yenye askari 3,000, imepewa nguvu kubwa zaidi kuliko vikosi vingine vya Umoja wa Mataifa vilivyowahi kutumwa kwenye shughuli za kulinda amani.

Brigedi hiyo iliundwa baada ya waasi wa M23 kuuvamia na kuukalia kwa muda mji wa Goma wenye wakazi wapatao milioni moja novemba mwaka jana. Waasi hao waliondoka katika mji huo Desemba 1,2012 chini ya makubaliano ya kusitisha mapigano.

Makundi kadhaa yenye silaha, ikiwemo M23, wanaendesha harakati zao za uasi mashariki mwa Kongo na wanapigania kuidhibiti nchi hiyo kubwa yenye maliasili za madini, kama vile dhahabu, urani, coltan, ambayo hutumika katika utengenezaji wa vifaa vingi vya elektroniki, ikiwemo simu za mkononi.

Waasi wa M23 waliuteka mji wa Goma Novemba 20, 2012 baada ya walinda amani kuondoka  katika mji huo wenye wakazi milioni moja. Wapiganaji wa M23 waliondoka katika mji huo Desemba 1,2013 baada ya makubaliano ya kusimamisha mapigano.

Waasi wa M23 walijiondoa katika jeshi la Kongo mwezi Aprili 2012 kupinga kile walichodai kuwa ni mwenendo mbaya ndani ya jeshi la Taifa (FARDC). Walikuwa wamejumuishwa katika jeshi chini ya mkataba wa amani uliosainiwa mwaka 2009.

Tangu mwezi Mei 2012, takriban watu milioni 3 wameyekimbia makazi yao katika eneo la mashariki mwa Kongo. Takriban watu milioni 2.5 ni wakimbizi wa ndani, huku zaidi ya watu 460,000 wamekimbilia katika nchi za Rwanda na Uganda.


Kongo imekuwa ikikabiliwa na matatizo matatizo kwa miongo kadhaa, kama vile umaskini uliokithiri, miondombinu mibovu, na vita katika eneo la mashariki mwa nchi hiyo ambavyo viliibuka tangu mwaka 1998 na kugharimu maisha ya zaidi ya watu milioni 5.5.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment