MURSI: NITAPAMBANA MPAKA “PUMZI YA MWISHO”

Ousted Egyptian President Mohamed Morsi 




Aliyekuwa Rais wa Misri, Muhammad Mursi, ameapa kupambana mpaka pumzi yake ya mwisho dhidi ya mapinduzi ya kijeshi yaliyomuondosha madarakani mwezi Julai mwaka huu.

Mapema jana, mmoja wa mawakili wa Mursi, bwana Mustafa Atteyah, alisema kuwa kiongozi huyo alifanya mazungumzo ya simu na familia yake kwa mara ya kwanza tangu jeshi lilipomuweka kizuizini.

Shirika la habari la Uturuki la Anadolu, lilikinukuu chanzo kilicho karibu na familia ya Mursi kikisema kuwa wakati wa mazungumzo hayo, Mursi aliiambia familia yake kuwa “ataendelea na msimamo wake mpaka pumzi ya mwisho”.

Kwa mujibu wa chanzo hicho, Mursi bado anajihesabu kuwa “rais halali” wa taifa hilo la kaskazini mwa Afrika.

Mazungumzo ya Mursi na familia yake yanakuja baada ya televisheni ya serikali kutangaza Septemba 14 kuwa kiongozi huyo aliyeuzuliwa atafikishwa mahakamani kujibu mashitaka ya “kuhamasisha mauaji na ghasia” zilizotokea mwezi Desemba 2012, baada ya pande mbili hasimu zilipopambana mjini Cairo.

Mgogoro ulishtadi nchini Misri tangu Julai 3 baada ya jeshi la nchi hiyo kumuondosha Mursi madarakani. Vilevile jeshi lilisitisha matumizi ya katiba na kulivunja bunge.

Mamia ya waandamanaji, wengi wao wakiwa wafuasi wa Mursi, waliuawa na kujeruhiwa katika ghasia mbaya zilizoikumba nchi hiyo kufuatia hatua hiyo ya jeshi.


Vikosi vya usalama vimeanzisha operesheni maalumu dhidi ya chama cha Mursi. Zaidi ya wafuasi 2,000 wa chama hicho wametiwa nguvuni tangu kuondolewa kwa Mursi, akiwemo kiongozi mkuu wa chama hicho, Muhammad Badie.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment