MISRI YAONGEZA MUDA WA HALI YA HATARI




RAIS wa mpito nchini Misri, Adly Mansour ameongeza muda wa hali ya hatari kwa muda wa miezi miwili zaidi kutokana na hali ya usalama kuendelea kuzorota.

Serikali imesema katika tangazo lililotolewa na Rais leo kuwa uamuzi huo umefikiwa kutokana na hali ya usalama ilivyo nchini humo.

Tangazo hilo linakuja siku kadhaa kabla ya kufikia kikomo kwa muda wa hali ya hatari uliowekwa mwezi Agosti.

Nchi hiyo bado inashuhudia maandamano ya kila siku yakitaka kurejeshwa madarakani kwa rais aliyeuzuliwa, Muhammad Mursi.

Awali serikali hiyo inayoungwa mkono na jeshi, ilitangaza hali ya hatari baada ya watu kadhaa kuuawa kufuatia vikosi vya usalama kuzivunja kambi mbili za waandamanaji waliokuwa wakimuunga mkono Mursi. Zaidi ya watu 1300, wengi wao wakiwa wafuasi wa Mursi, wameuawa katika ghasia zinazoendelea.

Serikali ya rais Mansour aliyeteuliwa na jeshi, ilianzisha operesheni ya kukabiliana na wafuasi wa Mursi na zaidi ya wanachama 2,000 wa vuguvugu la Udugu wa Kiislamu wametiwa korokoroni, akiwemo kiongozi mkuu wa vuguvugu hilo, Muhammad Badie.

Mauaji hayo yameamsha lawama za kimataifa na kuzitaka taasisi huru kufanya uchunguzi juu ya ghasia hizo.

Aidha, siku ya Jumatatu, Kamishina mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu, Navi Pillay, alitoa wito wa kufanyika uchunguzi wa mauaji hayo.

"Njia ya kuelekea kwenye uthabiti nchini Misri inategemea uthabiti wa utawala wa sheria katika hali inayohakikisha kuwa Wamisri wote, bila kujali mrengo wao wa kisiasa, jinsia, dini au wadhifa, wanatambuliwa kama wadau halali wa mustkbali wa nchi yao,” alisema.


Mwezi Julai, jeshi lilimuondoa madarakani Mursi, kusimamisha matumizi ya katiba na kulivunja bunge.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment