FALLUJAH: MJI ULIOATHIRIKA ZAIDI YA HIROSHIMA





Ni hivi karibuni tulishuhudia mataifa makubwa yakilumbana juu ya hatua inayotakiwa kuchukuliwa katika kuutia adabu utawala wa Rais Bashar al-Assad. Upande mmoja ulikuwa na nchi za Urusi, China, Iran na waitifaki wao. Huku upande wa pili ukiongozwa na Marekani, Uingereza, Ufaransa na waitifaki wao.

Upande wa Marekani ulikuwa ukishadidia kuchukuliwa hatua kali dhidi ya Damascus kwa hoja kwamba utawala wa Assad ulivuka “msitari mwekundu” kwa kutumia silaha za kemikali kuwaua raia katika shambulizi lililotokea katika viunga vya mji wa Damascus mnamo Agosti 21.

Baada ya shambulizi, tulimuona Rais Obama akiutangazia ulimwengu kuwa lazima Assad atiwe adamu kwa kushambuliwa kijeshi, na tukaona azma hiyo ikiwekwa vitendoni kwa kutuma manowari kadhaa katika bahari ya Mediterrania.

Kwa upande wa pili alikuwepo Urusi, China na Iran ambao walishikilia msimamo kuwa silaha hizo zilitumiwa na waaasi katika kutaka uungwaji mkono wa kimataifa na kutoa onyo kwa Marekani na waitifaki wake wasijaribu kuishambulia Syria nje ya kanuni za Umoja wa Mataifa.

Na ingawa moto umepoa baada ya muafaka uliofikiwa baina ya Urusi na Marekani wa kuziweka ghala za silaha za kemikali zinazomilikiwa na Syria chini ya udhibiti wa kimataifa na kisha kuziteketeza;

Na ingawa Assad alikubaliana na pendekezo hilo na hivyo kuepusha vita ambavyo vilitazamwa na baadhi ya wachambuzi wa mambo kama ujio wa “vita ya tatu ya dunia”,  na ambavyo vingeyagharimu maisha ya raia wasiokuwa na hatia; leo nimependa tujikumbushe kile kilichoachwa na Marekani katika mji mmoja wa Iraq baada ya kuivamia nchi hiyo kwa kisingizio cha kuzisaka silaha za nyuklia, zilizodaiwa kumilikiwa na rais wa wakati huo, marehemu Saddam Hussein. Mji huo ni Fallujah, mji unaopatikana umbali wa maili 30 magharibi mwa Baghdad. Lengo langu ni kujaribu kudodosa zile athari zinatokana na vita kama hivi kwenye miji mbalimbali duniani, na hususan Mashariki ya Kati.

Utafiti mpya uliotolewa hivi karibuni umebaini kuwa ongezeko la vifo vya watoto wachanga, saratani ya damu na matatizo mengine ya kiafya katika mji wa Fallujah nchini Iraq, ambao ulipigwa mabomu na Marekani mwaka 2004, ni zaidi ya kile kilichoripotiwa na manusura wa mabomu ya atomiki yaliyodondoshwa katika miji ya Hiroshima na Nagasaki nchini Japan mwaka 1945.

Madaktari wa Iraq mjini Fallujah wanalalamika kuwa tangu mwaka 2005 wameendelea kuhemewa na idadi ya watoto wanaozaliwa wakiwa na kasoro mbalimbali, kuanzia mtoto wa kike aliyezaliwa akiwa na vichwa viwili mpaka wale wanaozaliwa wakiwa wamepooza miguu na mikono. Pia wanasema kuwa walianza kushuhudia ongezeko la kutisha la watu wengi wenye saratani kuliko ilivyokuwa kabla ya vita ya Fallujah iliyopigwanwa baina ya vikosi vya Marekani na wapiganaji wa Kiiraq.

Madai ya madaktari hao yameungwa mkono na utafiti unaoonesha ongezeko la mara nne katika saratani zote na ongezeko la mara 12 kwa saratani ya watoto walio chini ya umri wa miaka 14. Vifo vya watoto wachanga katika mji huo viko juu mara nne zaidi ya ilivyo katika nchi jirani ya Jordan na mara nane zaidi ya Kuwait.

Dk. Chris Busby, ambaye ni profesa katika Chuo Kikuu cha Ulster na ambaye ni miongoni mwa waendeshaji wa utafiti huo uliowahusiha watu 4,800 mjini Fallujah, anasema kuwa ni vigumu kukificha chanzo halisi cha matatizo ya saratani na watoto wanaozaliwa wakiwa na upungufu katika viungo vyao. Anasema kuwa “ ili kuwa na athari kubwa kama hii lazima kiwango kikubwa sana cha kemikali kilitumika mwaka 2004 yalipoanza mashambulizi hayo.”

Meli za kivita za Marekani zilianza kuuzingira na kuutwanga kwa mabomu ambao upo maili 30 magharibi mwa Baghdad, mwezi Aprili 2004 baada ya wafanyakazi wanne wa kampuni ya ulinzi ya Kimarekani ya Black Water kuuliwa na miili yao kuchomwa moto. Baada ya miezi 8 ya kuwa mbali na mji, mwezi Nivemba mji huo ulivamiwa kwa kutumia vifaru na makombora ya angani yakatumika kuyalenga maeno ya waasi. Baadaye vikosi vya Marekani vilikiri kwamba vilitumia fosforasi nyeupe na sumu nyinginezo.

Katika mashambulizi hayo, makamanda wa Marekani, kwa kiasi kikubwa, waliifanya Fallujah kama eneo huru kutumia risasi ili kupunguza kiwango cha hasara na madhara kwa askari wao. Maafisa wa Kiingereza walishtushwa mno na hali ya kutozingatiwa madhara na hasara dhidi ya raia wa Fallujah. Kamanda mmoja wa Kiingereza, aliyekuwa akifanya kazi na vikosi vya Marekani mjini Baghdad, Brigedia Nigel Aylwin-Foster, anasema: “Wakati wa operesheni za awali Novemba 2004 mjini Fallujah, usiku mmoja mizinga 40 ilivurumishwa katika eneo dogo la mji huo.”

Kamanda huyo aliongeza kusema kuwa kamanda wa Kimarekani aliyeamuru matumizi hayo makubwa ya mashambulizi hakuona kuwa kuna umuhimu wa kuyatolea maelezo kwenye ripoti yake ya kila siku kwa mkuu wa majeshi wa Marekani. Dk Busby anasema kuwa ingawa hawezi kuanisha aina ya silaha zilizotumiwa na meli hizo, kiwango cha athari ya kijenitiki kilichowakumba wakazi wa mji huo kinaonesha kuwa katika maeneo kadhaa urani (uranium) ilitumika. Anasema: “Ninahisi kuwa walitumia silaha mpya kuyapiga majengo ili waweze kuzivunja kuta na kuwaua wale waliokuwa ndani ya kuta hizo.”

Uchunguzi huo ulifanywa na timu ya watafiti 11 mwezi Januari na Februari mwaka huu ambao walizitembelea nyumba 711 za mji wa Fallujah. Kwa kweli hali inatisha sana.


Uchunguzi huo ulibaini kuwepo kwa ongezeko la matatizo ya saratani na kasoro katika viungo vya watoto wanaozaliwa. Ilibainika kuwa vifo vya watoto wachanga ni 80 katika vizazi 1,000 ikilinganishwa na vifo 19 vya nchini Misri, 17 nchini Jordan na 9.7 nchini Kuwait. Ripoti inasema kuwa aina ya saratani hiyo ni “sawa na ile iliyopatikana kwa manusura wa shambulizi la mji wa Hiroshima nchini Japan, ambao waliathiriwa na mionzi yenye sumu kutoka kwenye bomu urani uliogunduliwa katika mabaki ya nyuklia.”

Watafiti waligundua kuwepo kwa ongezeko la mara 38 la kansa ya damu, mara 10 katika kansa ya matiti na ongezeko kubwa katika matatizo ya tezi na uvimbe wa ubongo. Hii ni tofauti na manusura wa Hiroshima ambao walikuwa na ongezeko la mara 17 katika kansa ya damu, lakini mjini Fallujah, wachunguzi hao wanasema kuwa tatizo sio tu kushamiri kwa kansa bali pia kasi kubwa ya ugonjwa huo unavyowaandama watu.

Katika utafiti huo kuna jambo la kushangaza. Utafiti ulibaini kuwa uwiano baina ya watoto wa kiume na wa kike wanaozaliwa umebadilika. Kabla ya mashambulizi hayo, uwiano ulikuwa watoto wa kiume 1,050 kwa watoto wa kike 1,000, lakini kwa wale waliozaliwa kuanzia mwaka 2005 vizazi vya watoto wa kiume vilishuka kwa asilimia 18, yaani uwiano ukawa watoto wa kiume 850 kwa watoto wa kike 1,000. Uwiano wa jinsia ni dalili ya kuwepo kwa athari ya kijenitiki inayowakumba wavulana zaidi ya wasichana. Mabadiliko kama hayo katika uwiano wa kijinsia yaligunduliwa pia baada ya tukio la Hiroshima.

Marekani iliamua kucha kutumia mashambulizi mazito nchini Iraq kuanzia mwaka 2007 kutokana na ghadhabu ya wananchi kutokana na vitendo vya jeshi lake. Lakini pia kulikuwa na anguko katika huduma za afya na usafi, kutokana na mashambulizi hayo. Athari ya vita iliyowakumba wakazi wa mji wa Fallujah ilikuwa kubwa na mbaya kuliko mji mwingine wowote nchini Iraq kwa sababu, baada ya mwaka 2004, mji huo uliendelea kuzingirwa na kutengwa na miji mingine ya nchi hiyo. Taathira za vita zilianza kurekebishwa taratibu sana. Hata hivyo wakazi wa mji huo walikuwa wakiogopa kwenda hospitalini mjini Baghdad kwa sababu ya vizuizi vingi vya kijeshi katika barabara iendayo katika mji mkuu huo wa Iraq.

Ikiwa huu ni mji mmoja tu wa Fallujah, vipi kuhusu miji mingine iliyokumbwa na zahma kama hizi?
Tafakari…

Kwa maoni: kabuga05@gmail.com


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment