Mfumo wa dijitali kurahisisha masomo waja


WANAFUNZI na walimu wa taasisi mbalimbali nchini wataanza kunufaika na mfumo wa teknolojia inayorahisisha uelewa wa haraka katika dhana ya kujifunza na kufundishia. Hayo yamebainika katika utiaji saini hati ya maridhiano ya kuweka kazi za mitaala kwenye mfumo wa dijitali kati ya Taasisi ya Elimu (TET) na Kampuni binafsi ya Media One, Dar es Salaam jana.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Utafiti, Habari na Machapisho wa TET, Makoye Wangeleja, alisema katika mfumo huo, wanafunzi wataweza kujifunza masomo mbalimbali ya darasani kwa kutumia michoro iliyotengenezwa kwa utaalamu mkubwa na kumfanya mwanafunzi kufurahia somo husika.

“Mfumo huu ni zaidi ya maabara za kawaida, kwa mfano wanafunzi wanaochukua masomo ya sayansi wataweza kuonyeshwa vitu kama vile moyo, ambao utawekwa kwa njia inayofanana na uhalisia, yakiwemo mapigo yake, jambo ambalo katika maabara za kawaida huwezi kuipata.

“Kwa njia hiyo wanafunzi watajifunza kwa vitendo na nadharia kwa pamoja, jambo ambalo litawaongezea uelewa na kupenda masomo husika,” alisema Wangeleja.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Media One, Anael Kihunwa, alisema mfumo huo utasaidia kurahisisha yasiyokuwa ya kawaida kuwa rahisi zaidi.

Alisema teknolojia hiyo itawasaidia vijana, hususan wanafunzi badala ya kutumia simu za mkononi kwa mambo ya muziki na starehe, wazitumie kujifunza masomo ya darasani.

Alisema programu hiyo itahusisha masomo yote, lakini kwa kuanzia watajikita zaidi katika masomo ya sayansi ambayo ni magumu tofauti na mengine.

Programu hiyo ni matokeo ya sera ya taifa ya Ushirikiano wa Serikali na Sekta binafsi (PPP), ambapo shule za sekondari na vyuo vya ualimu watanufaika kupitia mfumo huo.
CHANZO:MTANZANIA
Share on Google Plus

About mahamoud

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment