![]() |
| Waziri Mkuu wa Italia Mario Monti akiondoka katika kasri la Rais katika gari baada ya kukabidhi barua yake ya kujiuzulu kwa Rais wa nchi hiyo Giorgio Napolitano Disemba 21, 2012. |
WAZIRI Mkuu wa Italia Mario Monti amejıuzulu, siku chache baada ya waziri mkuu wa zamani Silvio Berlusconi na chama chake kutishia kuiangusha serikali yake.
Napolitano atalivunja bunge ndani ya siku chache zijazo, na uchaguzi wa kitaifa utafanyika mwezi Februari.
Monti, aliyewahi kuwa kamishina mwandamizi wa Umoja wa Ulaya, ataendelea kubaki katika siasa za nchi hiyo.
Hatua yake hiyo inakuja baada ya mapema mwezi huu Berlusconi na chama chake cha mrengo wa kulia (PDL), ambacho ndio chama kikubwa kabisa katika bunge la Italia, kutishia kusitisha uungaji mkono wao kwa serikali ya Monti kufuatia anguko kubwa la uchumi katika nchi hiyo.
Monti ametangaza kujiuzulu kwake mwaka mmoja baada ya kushika nafasi iliyoachwa mtangulizi wake aliyekuwa amendamwa na kashfa nyingi, Silvio Berlusconi, ambaye alilazimika kujiuzulu kutokana na mgogoro wa madeni ulioikumba Italia.
Monti, ambaye aliwataka Waitalia kujitoa "mhanga" katika kukabiliana na mgogoro wa madeni na mtikisiko wa kiuchumi, alishuhudia umaarufu wake ukishuka kwa kasi kutoka asilimia 60 wakati akiingia madarakani mpaka asilimia 30 katika wiki za hivi karibuni.
Waziri mkuu huyo anayeondoka aliwahi kusema kuwa Italia ilihitaji kumeza "dawa chungu zaidi" kwa sababu "aspirin" isingeweza kuurejesha uchumi katika hali ya kawaida baada ya miaka kadhaa ya uongozi mbovu.
Monti ameashiria kuwa anaweza kuongoza serikali ya muungano wenye mrengo wa kati iwapo uchaguzi wa mwezi Februari 2013 hautatoa ushindi wa wazi.
Monti aliwahi kuhudumu kama mwenyekiti wa Tume ya pande tatu ya Umoja wa Ulaya kuanzia mwaka 2010 mpaka 2011.
CHANZO: GVN/HGL

0 comments:
Post a Comment