VIONGOZI WA KIARABU WAITAZAMIA MAREKANI KUTANZUA MGOGORO KATI YAO



Gulf leaders look to US to resolve inter-Arab dispute
 Kiongozi wa Kuwait Sheikh Sabah al-Ahmad Al-Sabah (mbele) akihudhuria ufunguzi wa mkutano wa 38 wa viongozi wa Baraza la Ushirikiano wa Ghuba (GCC) kwenye kasri la Bayan mjini Kuwait, mnamo Desemba 5, 2017.



DOHA, Qatar

Mlolongo wa ziara zinazotarajiwa kufanywa na viongozi wa mataifa ya Ghuba nchini Marekani unaonekana kuwa unalenga kutengeneza mazingira mazuri ya mkutano mkubwa kati ya Marekani na Ghuba unaotarajiwa kufanyika mwezi Mei.

Kwa mujibu wa maafisa wa ngazi za juu wa Kiarabu, mkutano huo unalenga kutanzua mgogoro wa kisiasa uliodumu kwa miezi kadhaa kati ya Qatar na na mataifa manne ya Kiarabu yakiongozwa na Saudi Arabia.
Mrithi wa kiti cha Ufalme wa Saudia, Mohammad bin Salman, anatarajiwa kufanya ziara mjini Washington mnamo Machi 19. Mwezi mmoja baadaye kiongozi wa Qatar, Tamim bin Hamad Al Thani naye anatarajia kufanya ziara kwenye mji mkuu huo wa Marekani.

Akizungumza kwenye televisheni ya taifa mapema Jumatano, Naibu Waziri wa mambo ya nje wa Kuwait Khaled al-Jarallah alisema kuwa ziara hizo zinalenga kuandaa mazingira kwa ajili ya mkutano huo.

"Kuna matumaini ya kufanyika mkutano wa kilele nchini Marekani kwa lengo la kutanzua mgogoro wa uhusiano kati ya mataifa ya Kiarabu," alisema bwana al-Jarallah. "Lakini mialiko bado haijatumwa."

"Mgogoro huu lazima utatulie kwa njia moja au nyingine ili sisi [Mataifa ya Kiarabu] tuweze kushughulikia kwa pamoja changamoto nyingi zinazolikumba eneo letu hili," aliongeza.

"Marekani inalitambua hili na – kama ilivyo kwa Kuwait – inataraji kukomeshwa kwa mzozo huu ili iweze kuweka nguvu moja kwa moja katika kuzikabili changamoto hizi," alisema al-Jarallah.

Wiki hii, Naibu Waziri wa Marekani anayeshughulikia masuala ya Ghuba Timothy Lenderking, pamoja na jenerali wa zamani wa jeshi la wanamaji la Mareni Anthony Zinni, walifanya ziara maalum katika mataifa ya Kiarabu ambayo iliwapeleka Kuwait, Qatar, Misri, Saudi Arabia, Bahrain na Oman.

Ziara hiyo iliripotiwa kuwa na lengo la kutafuta suluhu ya mzozo wa eneo la Ghuba na kuandaa mazingira ya mkutano wa kilele unaotarajiwa kufanyika mwezi Mei.

Mwaka jana, Saudi Arabia na waitifaki wake wanaojumuisha mataifa ya Falme za Kiarabu, Misri na Bahrain, kwa pamoja walikata uhusiano na Qatar, wakiituhumu Doha kuwa inaunga mkono makundi ya kigaidi katika ukanda huo.

Mataifa hayo yalitishia kuiwekea vikwazo zaidi Qatar iwapo itashindwa kutekeleza masharti iliyopewa, ikiwa ni pamoja na kutakiwa kukifunga kituo cha matangazo cha Al Jazeera chenye makao yake mjini Doha.

Hata hivyo, Qatar iliyakataa masharti hayo na kukana vikali tuhuma zilizoelekezwa dhidi yake.
  
Nayo Kuwait kwa upande wake imeendelea kutoegemea upande wowote kwenye mzozo huo huku ikijitahidi kuwa mpatanishi katika mzozo huo.



Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment