JESHI PAKISTAN LAPEWA AMRI KUZITUNGUA NDEGE ZA MAREKANI


The file photo of a US drone
Ndege ya Marekani isiyokuwa na rubani (drone)

Kufuatia hali ya sintofahamu iliyoukumba uhusiano wa Washington na Islamabad, Pakistan imeviamuru vikosi vyake vya anga kuzitungua ndege zozote zisizokuwa na rubani (drones) zitakazoingia katika anga ya nchi hiyo, zikiwemo zile za jeshi la Marekani ambazo zinasadikiwa kuhusika na idadi kubwa ya vifo vya raia katika taifa hilo la Asia.

“Hatutoruhusu yeyote kukiuka sheria za anga yetu. Nimetoa amri kwa PAF (jeshi la anga la Pakistan) kuzitungua droni, zikiwemo zile za Marekani, kama zitaingia anga yetu, na kwenda kinyume na uhuru wa nchi yetu na mshikamano wa eneo letu,” Mkuu wa kikosi cha anga cha nchi hiyo, Sohail Aman amesema katika taarifa yake mjini Islamabad, kama ilivyoripotiwa na mtandao wa Times of India.

Amri hiyo ni tofauti na sera ya mwanzo ya jeshi la anga la nchi hiyo, ambapo lilikuwa likilalamikia mashambulizi ya droni za Marekani kwenye ardhi yake, lakini halikuwahi kutoa kitisho cha kuzitungua.

Tangazo hilo linakuja wiki mbili baada ya droni moja ya Marekani kushambulia eneo linaloshukiwa kuwa kambi ya wanamgambo katika mpaka wa nchi hiyo na Afghanistan na kuua watu wasiopungua watatu.

Marekani imekuwa ikitumia ndege zisizokuwa na rubani kufanya upelelezi na mashambulizi nchini Pakistan tangu Washington na washirika wake walipoivamia Afghanistan mwaka 2001.

Kwa mujibu wa takwimu za Ofisi ya Habari za Kiuchunguzi, mamia ya raia, wakiwemo wanawake na watoto, wameuawa katika mashambulizi ya droni za Marekani yanayolenga kile kinachoelezwa kuwa ni maeneo ya wanamgambo nchini Pakistan na Afghanistan tangu mwaka 2004.

Islamabad imekuwa ikilaani mashambulizi ya droni za Marekani kwenye ardhi yake, ikiielezea kuwa ni kukiuka uhuru wa Pakistan.

Operesheni ya droni za Washington imekuwa ikipingwa vikali na wananchi wa Pakistan ambao wamefanya maandamano kadhaa kwa miaka kadhaa kupinga vifo vilivyosababishwa na mashambulizi hayo.


Waandamanaji wa Kipakistan wakichoma moto bendera ya Marekani wakati wa maandamano ya kulaani shambulizi la droni ya Kimarekani mnamo Mei 27, 2016 mjini Peshawar. 


Kamanda Aman alikumbushia pia tukio la kuvunja uaminifu kuhusu ndege aina ya F-16 zilizotengenezwa na Marekani ambazo Pakistan ilizilipia, lakini hazikutolewa.

Kamanda huyo wa jeshi la anga la Pakistan alisifu uwezo wa kikosi chake akisema kuwa wanajeshi wake wako tayari kulinda uhuru wa nchi hiyo.

Amri hiyo mpya kabisa imekuja kufuatia sintofahamu iliyojitokeza kwenye uhusiano wa washirika hao wawili kufuatia shutuma za Rais wa Marekani Donald Trump dhidi ya Islamabad akiituhumu kuunga mkono makundi ya wanamgambo.

Maafisi mjini Islamabad wamekanusha vikali tuhuma hizo. Wanasema kuwa Pakistan imefanya kazi kubwa kupambana na ugaidi.

Mwezi Agosti Trump aliikosoa vikali Pakistan wakati akitangaza mkakati mpya wa utawala wake nchini Afghanistan. Kauli za rais huyo ziliibua hasira miongoni mwa maafisa na wananchi wa Pakistan.



Aidha, amri hiyo imekuja wiki moja baada ya ziara iliyofanywa na Waziri wa Ulinzi wa Marekani Jim Mattis nchini humo ambapo aliwataka kuongeza mara dufu juhudi zao za kupambana na wanamgambo ambao wanashukiwa kuitumia nchi hiyo kama ngome yao na kufanya mashambulizi katika nchi jirani ya Afghanistan.


Waziri wa Ulinzi wa Marekani James Mattis (kushoto) akiwasili mjini Islamabad, Pakistan, Desemba 4, 2017.


Mattis pia alikutana na maafisa wa ngazi za juu wa jeshi la Pakistan, akiwemo mkuu wa jeshi Jenerali Qamar Javed Bajwa na Luteni Jenerali Naveed Mukhtar, ambaye ni mkuu wa shirika mama la ujasusi ambaye serikali ya Marekani inasema kuwa ana uhusiano na wanamgambo wa Haqqani na Taliban.

Afisa mmoja kutoka wizara ya ulinzi ya Marekani, akizungumza kwa sharti la kutotajwa jina, alinukuliwa na taarifa za vyombo vya habari akisema kuwa mazungumzo ya Mattis alikuwa ya moja kwa moja na ya wazi.

Aliongeza kuwa miongoni mwa mambo yaliyojadiliwa ni kuifanya Pakistan isaidie kuwaleta wanamgambo wa Taliban kwenye meza ya mazungumzo.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment