MAKAMU WA RAIS WA GAMBIA AJIUZULU

Gambia’s vice president Isatou Njie Saidy
Makamu wa Rais wa Gambia Isatou Njie Saidy



Makamu wa Rais wa Gambia amejiuzulu kufuatia kushitadi kwa mgogoro wa kisiasa katika taifa hilo la Afrika Magharibi uliochochewa na hatua ya Rais Yahya Jammeh kukataa kung’atuka licha ya kushindwa na mpinzani wake Adama Barrow katika uchaguzi wa mwezi Desemba.

Isatou Njie Saidy, ambaye ni afisa wa ngazi ya juu kabisa kuitupa mkono kambi ya Jammeh, alitangaza uamuzi wake huo Jumatano, saa chache kabla ya muda wa utawala wa Jammeh kufikia tamati. Amekuwa makamu wa rais wa Gambia tangu mwaka 1997.

Siku hiyo hiyo Waziri wa Elimu Abubacar Senghore alitangaza kujiuzulu na kuwa waziri wa nane kuitupa mkono serikali ndani ya mwezi huu.

Awali Jammeh aliyakubali matokeo ya uchaguzi wa Desemba 1, 2016, ambapo Barrow alitangazwa kuwa mshindi, lakini baadaye akabadili msimamo wake na kuwasilisha mashitaka yake kwenye Mahakama Kuu akilalamikia hitilafu katika uchaguzi huo.

Nchi kadhaa za eneo hilo ambazo zimekuwa zikijaribu kusuluhisha mgogoro huo zimetishia kuingia kijeshi iwapo Jammeh atakataa kung’atuka pindi muhula wake wa utawala utakapofikia kikomo leo usiku wa manane.

Senegal, ambayo inaizunguka sehemu kubwa ya Gambia, imeshapeleka vikosi kwenye mpaka wake na Gambia huku ikiziweka tayari ndege zake za kivita ili kumg’oa Jammeh.


Wakati huo huo, Barrow ametangaza kuwa ataapishwa kama rais halali wa Gambia katika ubalozi wa nchi hiyo mjini Dakar, Senegal. Amekuwa nchini Senegal tangu siku ya Jumapili baada ya viongozi wa Kiafrika wanaomuunga mkono kumualika kuhudhuria rasmi kwenye mkutano wa mataifa hayo.



Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment