MKONGWE WA MASUMBWI MUHAMMAD ALI AFARIKI DUNIA


 Boxing legend Muhammad Ali dies at age 74

Mkongwe wa masumbwi duniani Muhammad Ali amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 74, msemaji wa familia amethibitisha.

Bingwa huyo aliyewahi kutwaa taji la uzito wa juu mara tatu alikuwa amelazwa katika hospitali huko Phoenix katika jimbo la Arizona nchini Marekani tangu siku ya Alhamisi  kwa tatizo la kushindwa kupumua.

Pia Ali alikuwa akisumbuliwa na maradhi ya Parkinson tangu mwaka 1984. Mshindi huyo wa medali ya dhahabu katika mashindano ya Olympic alikuwa na tatizo la upumuaji ambalo linahusishwa na ugonjwa huo wa Parkinson.

“Baada ya miaka 32 ya kupambana na ugonjwa wa Parkinson, Muhammad Ali ametutoka akiwa na umri wa miaka 74, msemaji wa familia Bob Gunnell amesema katika taarifa yake.

“Familia ya Ali ingependa kuwashukuru wote kwa mawazo, dua na uungaji mkono wenu na inaomba faragha kwa wakati huu”.

Mazishi ya Ali yatafanyika katika mji wake wa Louisville, Kentucky. 

Mapema kabla ya mauti yake, Gunnell alikuwa amesema kuwa Ali alikuwa katika hali ya kawaida katika hospitali ambayo haikuwa imewekwa wazi katika mji wa Phoenix.

Muhammad Ali alizaliwa katika mji wa Louisville mwezi Januari mwaka 1942 na jina lake la awali ni Cassius. Alianza masumbwi akiwa na umri wa miaka 12 na kushinda taji la uzito wa juu mwaka 1964. Mwaka huohuo alibadili dini kuwa Muislamu akabadili jina lake na kuwa Muhammad Ali.

Kabla ya kustaafu masumbwi mwaka 1981 alishinda mataji mengine mawili ya uzito wa juu.

Muhammad Ali anachukuliwa kama mmoja wa wanamichezo wakubwa kabisa wa karne ya 20 na mwanamasumbwi wa uzito wa juu wa wakati wote. Anajulikana kwa mtindo wa upiganaji wake usiokuwa wa kawaida ambao ulijumuisha kasi ya ajabu, wepesi, nguvu na radiamali endelevu dhidi ya wapinzani wake.

(Mzizima WhatsApp: +255 712 566 595)



Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment