URUSI NA MAREKANI ZAZIDI KUVUTANA JUU YA SYRIA

A picture released by the Syrian Arab News Agency on September 12, 2015, shows a Russian plane carrying humanitarian aid being unloaded on the tarmac of the Martyr Bassil al-Assad international airport in Latakia, Syria. (AFP)
Ndege ya Urusi ikipakua shehena mjini Latakia, Syria, Septemba 12, 2015.



Maafisa wa Marekani wamefichua kuwa Urusi inatumia anga ya Iran na Iraq kupeleka zana za kijeshi na askari nchini Syria, na hivyo kuongeza mvutano baina yake na Marekani.

Kwa mujibu wa ripoti moja, kwa uchache ndege kubwa za usafirishaji wa zana za kijeshi aina ya Antonov An-124 ziliondoka kutoka kambi moja nchini Urusi wiki moja iliyopita kwa lengo la kupeleka zana za kijeshi nchini Syria kwa kutumia anga za Iran na Iraq, gazeti la New York Times limeripoti leo Jumatatu kwa kuwanukuu maafisa wa Marekani.

Maafisa hao wameliambia gazeti hilo kuwa ndege hizo zimetua katika uwanja mmoja wa ndege katika jimbo la Latakia magharibi mwa Syria.

Kwa mujibu wa taarifa za kintelejensia za Marekani, meli za kijeshi na makombora ya Urusi vinaulinda uwanja huo wa kijeshi huko Latakia.

Kwa kutumia njia mpya ya anga, Moscow inapuuza juhudi za Washington kuzuia usafirishaji huo na jambo hilo linaongeza mvutano baina ya mataifa hayo.

Awali ikulu ya Marekani ilikuwa na matarajio kuwa imezuia harakati za Urusi kupeleka zana za kivita na wanajeshi nchini Syria baada ya Bulgaria ambayo ni mwanachama wa NATO kutangaza kuwa usingeruhusu anga yake kutumiwa na Urusi.

Lakini kwa haraka sana, Urusi ilianza kurusha ndege zake kuelekea Iran na Iraq, huku Waziri wa mambo ya nje wa nchi hiyo, Sergey Lavrov, akisema jana Jumapili kuwa wataendelea kufanya hivyo licha ya upinzani wa Marekani.


“Usafirishaji wa zana za kijeshi ulikuwepo, unafanyika na utaendelea kufanyika,” alisema bwana Lavrov kama alivyonukuliwa na mashirika ya habari ya Urusi. “Zana hizo zinasindikizwa na wataalamu wa Urusi, ambao husaidia kuziandaa, kuwapa mafunzo askari wa Syria namna ya kuzitumia.”

Lavrov aliongeza kuwa Moscow itaendelea kuipa silaha serikali ya Syria katika vita vyake dhidi ya wanamgambo wa kundi la Dola ya Kiislamu, akizitaka nchi nyingine kuchukua msimamo kama huo na kuisaidia Damascus katika vita hivyo.

Utawala wa Obama umeionya Moscow na kuitaka iweke ukomo wa usafirishaji wa zana za kijeshi nchini Syria.

Juzi Jumamosi, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani, John Kerry, alimpigia simu Lavrov na kuonya kwamba Washington ina wasiwasi mkubwa kuhusu ripoti za Urusi kujijenga kijeshi katika eneo hilo.

Migogoro iliyotokea katika mataifa ya Syria na Ukraine yameibua mvutano baina ya Urusi na mataifa ya Magharibi. Moscow na Washington zimekuwa na tofauti kubwa kuhusu migogoro ya Syria na Ukraine.

Syria ilitumbukia katika machafuko tangu mwezi Machi mwaka 2011. Maelfu ya raia wamepoteza maisha huku wengine milioni 10 wakiwa ukimbizini.


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment