WASIFU WA MGOMBEA URAIS KWA CHAMA CHA ACT WAZALENDO

Mama Anna Mghwira katika harakati za kisiasa

MAMA ANNA ELISHA MGHWIRA.

Mgombea Urais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania 2015 kwa tiketi ya ACT WAZALENDO.

Chama cha ACT Wazalendo kimemteua na kumpitisha Mama Anna Mghwira kuwa mgombea Urais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 25, 2015. Pia kimemteua na kumpitisha Ndugu Hamad Mussa Yusuf kuwa mgombea mwenza wake.

Mama Anna Mghwira ambaye ni Mwenyekiti Taifa wa chama cha ACT Wazalendo, anakuwa mwanamke wa pili kuwania nafasi ya Urais katika historia ya siasa za Tanzania.

NI NANI HUYU Anna Elisha Mghwira?

Mama Anna Mghwira alizaliwa Januari 23, 1959 katika hospitali ya Mkoa wa Singida, kata ya Mungumaji, kitongoji cha Irao, Manispaa ya Singida Mjini.
Baba mzazi wa Anna alikuwa Diwani na kiongozi wa TANU kabla ya CCM hadi mwaka 1985, mama yake alijishughulisha na kilimo na ufugaji na wazazi hawa kwa ujumla walipata watoto tisa akiwemo Anna.

Alianza safari ya kielimu katika shule ya Msingi Nyerere Road mwaka 1968 - 1974 akaendelea na Sekondari kwenye shule ya Ufundi Ihanja kati ya mwaka 1975 - 1978 kabla ya kuhitimisha masomo ya juu ya Sekondari (kidato cha Tano na Sita) Lutheran Junior Seminary mwaka 1979 - 1981.
Mwaka 1982 alijiunga na Chuo Kikuu cha Theolojia cha Tumaini na kuhitimu Shahada ya Theolojia mwaka 1986.

Mwaka huohuo 1986 alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambako alisoma na kuhitimu Shahada ya Sheria (LLB).
Aliendelea na shughuli za ujenzi wa Taifa akifanya kazi ndani na nje ya Tanzania na kupata uzoefu mkubwa.

Mwaka 1999 alijiunga na Chuo Kikuu cha Essex, nchini Uingereza na akatunukiwa Shahada ya Uzamili ya Sheria (LLM) mwaka 2000.
Licha ya kuwa mwanatheolojia na mwanasheria aliyebobea pia amefanya kazi za maendeleo kwa muda mrefu na ana uzoefu katika uendeshaji wa Serikali za Mitaa, Utumishi katika Mashirika ya Kitaifa, Kimataifa, mashirika ya dini ambamo amejihusisha na Masuala ya Wanawake, Watoto, Wakimbizi, Utawala Bora na Haki za Binaadamu.

Mama Anna Mghwira ana historia ya kupenda siasa, masuala ya jamii na michakato ya maendeleo kama inavyojidhihirisha katika maandiko yake mbalimbali katika safu za magazeti na majarida ndani na nje ya Tanzania. Jambo hili linampambanua Anna na wagombea wengine ambao hawaandiki chochote na hata hotuba zao huandikiwa.

Alianza siasa Tangu wakati wa TANU akiwa mwanachama wa Umoja wa Vijana wa TANU (TANU YOUTH LEAGUE) na aliwahi kushinda tuzo mbalimbali kutokana na ushiriki wake wa juu katika TANU lakini baadae ilipoanzishwa CCM alipunguza ushiriki wake ili ajipe muda zaidi katika masomo na baadae Ndoa na Malezi ya watoto.




Aliolewa na Shedrack Mghwira tangu mwaka 1982 na walibahatika kupata watoto watatu wa kiume Fadhil, Peter na Elisha. Hata hivyo kwa bahati mbaya, mumewe kwa hivi sasa ni marehemu.
Kwa muda mrefu hakuwa akijihusisha na siasa mpaka mwaka 2009 ambako alijiunga na chadema na kushika nyadhifa za Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake ngazi ya Wilaya na Katibu wa Baraza la Wanawake ngazi ya Mkoa.

Machi 2015 alijiunga na chama kipya cha ACT Wazalendo na Machi 28, 2015 Mama Anna Mghwira aliingia kwenye historia ya siasa za mageuzi Tanzania baada ya Mkutano Mkuu wa Kwanza wa Chama Cha ACT Wazalendo kumchagua kwa kura nyingi kuwa Mwenyekiti Taifa wa Kwanza wa chama hicho na pia Mwanamke wa Kwanza katika historia ya siasa za Tanzania kuwa Mwenyekiti Taifa wa chama cha Siasa.

Agosti 20, 2015 Mkutano Mkuu wa Kidemokrasia wa Chama cha ACT Wazalendo ulimteua na kumpitisha kuwa mgombea wa nafasi ya Urais akipeperusha bendera ya chama hicho.
Agosti 21, 2015 amechukua fomu na kukamilisha taratibu zote za kisheria na kuteuliwa Rasmi na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (National Electoral Commission) kumthibitisha kama mgombea Urais rasmi wa Chama cha ACT Wazalendo.

Mama Anna Mghwira hana madoadoa ya ufisadi na wala hahitaji dodoki la kumsafisha. Ni mtu mwenye uwezo na sifa za kuwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwa kazi za Rais ambazo ni kufikiri, kuwa mlinzi Mkuu wa Umoja, Amani na Tunu za Taifa na kuwa mfano bora wa ubinaadamu anazimudu.


Akizungumzia uteuzi wake kwa nafasi hiyo Mama Anna anasema: "Taifa linahitaji kiongozi mwenye moyo wa nyama, mwenye upendo, maono, uadilifu, uzalendo na mwenye uwezo wa kuwaunganisha watu wote bila upendeleo na huyo sio mwingine bali ni Ndugu Anna Elisha Mghwira".
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment