WENYE MABUSHA MTWARA WASUSWA NA HOSPITALI YAO YA MKOA, WAPONEA MSUMBIJI

 Mabusha

HOSPITALI ya Rufaa ya Mkoa wa Mtwara, Ligula, imesusa kuwapokea wagonjwa wa Mabusha, wanaohitaji kufanyiwa upasuaji kupitia Mradi Maalumu wa Serikali, hivyo kuwalazimu baadhi ya wagonjwa hao kufuata huduma hiyo nchini Msumbiji.

Taarifa za uhakika zilizopatikana hospitalini hapo kabla ya kuthibitishwa na baadhi ya wananchi ama wanaosumbuliwa na ugonjwa huo au jamaa wa wagonjwa hao kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa huo wa kusini mwa Tanzania unaopatikana na Msumbiji, zinasema uongozi wa hospitali hiyo uligoma kuwapokea wagonjwa wa aina hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, kutokana na hali hiyo, baadhi ya wagonjwa wa aina hiyo mkoani humo, ambao walilengwa kuwa wanufaika wa mradi maalumu wa kupambana na magonjwa ya mabusha na matende nchini, walilazimika kukimbilia Msumbiji ili kupata huduma hiyo, ambayo kama Tanzania nchi hiyo nayo ilikuwa na mradi huo kwa udhamini wa Shirika la Afya Duniani (WHO).

Mganga Mkuu Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Ligula, Mkoa wa Mtawara, Dk. Mohamed Gwao, alipoulizwa kuhusiana na madai hayo ya kuwakataa wagonjwa wa aina hiyo kupitia mradi huo maalumu wa Serikali, alikataa kuingia kwa undani kuzungumzia suala hilo, akisema hana taarifa yoyote inayohusu wagonjwa wa mabusha kunyimwa matibabu hospitalini kwake hapo.

Hata hivyo, Dk. Gwao amekiri kuwepo kwa mradi wa kupambana na magonjwa ya mabusha na matende, akisema ulikuwa unasimamiwa moja kwa moja na Maofisa wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.

Baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Dindwa, kilichoko Kata ya Kitaya, Wilaya ya Mtwara Vijijini, miongoni mwao wakiwemo waliojitambulisha kwa majina ya Twahiru Godson na Issa Sadiki, wamethibitisha kuwepo kwa wananchi wengi wa mkoa huo waliokuwa wakikabiliwa na ugonjwa huo waliokosa huduma hiyo, ambayo tiba yake inahusisha upasuaji.

Katika jitihada za kudhihiti ugonjwa wa mabusha, maarufu kwa jina la Ngiri Maji pamoja na matende, ugonjwa ambao unaelezwa kuenea zaidi katika mikoa ya mwambao wa Bahari ya Hindi, hasa mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Tanga, Lindi na Mtwara, Serikali, kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ilizindua kampeni maalumu, takriban miaka minne iliyopita, kwa ajili ya kutoa huduma ya matibabu bure kwa wananchi wanaosumbuliwa na magonjwa hayo katika maeneo hayo.

Takwimu kutoka serikalini zinaonyesha kwamba katika kipindi cha miaka minane iliyopita, wananchi wanaofikia milioni 10, walipatiwa kinga ya magonjwa hayo nchi nzima.

Habari kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii pamoja na Taassisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) zinaeleza kwamba mpango huo wa kutoa kinga ya kuzuia maambukizi pamoja na kutoa huduma kwa waathirika wa magonjwa ya Ngiri maji na Matende, bado unaendelea unaendelea nchini kote, ukilenga kuhakikisha kuwa maradhi yote hayo yanateketezwa nchini hadi kufikia mwaka 2020.


CHANZO: Mtandao wa Fikra Pevu
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment