RISASI ZATIKISA KATIKA MSIKITI MJINI MOMBASA





Milio ya risasi imesikika leo ndani na nje ya msikiti wa Masjid Mussa katika mji wa Mombasa nchini Kenya kufuatia hatua ya polisi kuvamia msikitini hapo kutokana na kile walichosema kuwa ni kupokea taarifa kwamba kuna vijana wa Kiislamu waliokuwa wakipewa mafunzo ya kijeshi na kasumba za misimamo mikali.

Hatua hiyo ya polisi iliibua ghasia ndani ya msikiti huo wa Masjid Mussa uliopo katika maeneo ya Majengo na katika mitaa ya jirani. Polisi walifyatua gesi ya kutoa machozi na kumekuwepo na taarifa kuwa risasi za moto zilitumika kuudhibiti umati wa watu waliokuwa wakiwarushia mawe polisi.

Milio ya risasi iliendelea kusikika saa nne baada ya polisi kuingia mahali hapo na mwangwi wa milipuko ulitanda katika mitaa ya jirani.

Shirika la habari la Reuters limemkariri mkuu wa polisi katika mkoa wa Mombasa, Robert Kitur akisema kuwa polisi walivamia eneo hilo baada ya kutonywa juu ya uwepo wa vijana hao. Na kwamba maafisa wa polisi walipofika hapo walishambuliwa. Hata hivyo, maelezo ya mkuu huyo wa polisi hayajathibitishwa na vyanzo huru.

"Tumewakuta wakiwajaza vijana kasumba za misimamo mikali na mafunzo mbalimbali,” Kitur aliwaambia waandishi wa habari jirani na msikiti huo wakati operesheni hiyo ikiendelea.

Waislamu wengi katika mitaa ya Mombasa wanahisi kunyanyapaliwa na serikali ya Kenya na operesheni zinazofanywa na serikali hiyo katika kukabiliana na kile inachodai kuwa ni mitandao ya mafunzo ya kijeshi zimekuwa zikiibua ghasia katika mji huo wa kitalii.


Lakini maafisa usalama nchini humo wanadai kuwa Masjid Mussa imekuwa ikitoa mafunzo kwa wanamgambo ambao huenda kuungana na wapiganaji wa al Shabaab nchini Somalia.

Mwezi Agosti 2012 watu waliojifunika nyuso walimuua kwa kumpiga risasi Imamu  wa Msikiti huo, Sheikh Aboud Rogo, aliyekuwa akitoa mahubiri hapo na ambaye serikali za Marekani na Kenya zilikuwa zikimshutumu kutoa mafunzo na kufadhili waasi wa al Shabaab nchini Somalia wenye mafungamano na mtandao wa wapiganaji wa al Qaeda.

Mwaka mmoja baadaye, mrithi wa sheikh Rogo, Sheikh Ibrahim Rogo aliuawa katika shambulizi kama hilo. Matukio yote mawili yaliibua ghasia katika mji huo.

Waumini katika msikiti huo wanawatuhumu wanausalama kuhusika na vifo hivyo, shutuma ambazo polisi wamekuwa wakizikanusha.


Kamanda Kitur anasema kuwa askari wamewakamata zaidi ya watu 100 katika operesheni ya leo na maafisa wawili wamejeruhiwa.

CHANZO: http://www.reuters.com/article/2014/02/02/us-kenya-riot-idUSBREA110A220140202
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment