JINSI YA KUIGUNDUA PICHA BANDIA KWENYE MITANDAO YA KIJAMII

 


Miongoni mwa vitu vizuri sana kuhusu mitandao ya kijamii ni uhuru na urahisi wa kubadilishana taarifa. Hata hivyo, uhuru huo una gharama zake. Katika ulimwengu wa mitandao ya kijamii isiyochujwa, sio kila taarifa ni ya kweli.

Picha ni rahisi sana kubadilishwa, kurekebishwa na kutumika nje ya muktadha uliokusudiwa. Ili kuepuka kuangukia katika mtego wa kudanganywa na ufundi mbalimbali wa upotoshaji wa taarifa, tunahitaji kuyafumbua macho na akili zetu zaidi.

1. Una uhakika kuwa ni kweli?

Wakati fulani zinapotokea taarifa motomoto na za ghafla kama vile janga fulani, tukio la kusikitisha, mijadala ya kisiasa, vurugu, ghasia, mauaji, maandamano na kadhalika, akili zetu hutahamaki na kuwa na mwelekeo wa kuamini kile tunachokiona kwenye vyombo vya habari, iwe televisheni, kompyuta, simu, magazeti na kadhalika.

Hata hivyo, jambo la busara ni kujizuia na kuziangalia tena hizo picha ili kuwa na uhakika kuwa ni picha halisi au ni za kweli.

Picha unayoiona inawezekana ikawa haijahaririwa na ikawa picha halisi, lakini una uhakika kuwa imeoneshwa kwenye muktadha halisi au tukio halisi? Inawezekana ilipigwa wakati tofuati na kwenye tukio tofauti na hilo unaloliona. Sasa kwa kuwa uwezo wa kugundua ni kipi sahihi na kipi sio sahihi unaweza kuwa umetamalakiwa na mshtuko au taathira ya tukio hilo, tumia muda wa ziada kupata uhakika na uthibitisho wa kile unachokiona.

2. Ni nani aliyetuma hiyo picha?

Je, unamjua mtu aliyetuma hiyo picha? Je, unamuamini? Kama humjui, basi njia nzuri ya kujua kama mtu huyo anaaminika au la kwa kuangalia ujumbe au picha za nyuma alizowahi kuzituma kwa watu. Kama akaunti yake ni mpya kwako, basi kuwa makini! Kama picha ya kwenye ubao wa wasifu wake (profile) haikupi taswira nzuri, basi ni bora kuwa na tahadhari.


3. Je, picha imefanyiwa mabadiliko na marekebisho?

Unapoitazama picha kwa mara ya kwanza unaweza kudhani ni picha halisi, lakini itazame tena. Je, unaona hitilafu zozote kwenye kivuli au jinsi inavyoakisi? Njia bora kabisa ni kuangalia iwapo picha hiyo imefanyiwa mabadiliko ni kuangalia mwanga.

Kuna njia rahisi ya kuiangalia picha hiyo iwapo unatumia programu ya  ‘Photoshop’. Bonyeza Image > Adjustments > Hue/Saturation na kisha hamisha  viwango vya Hue/Saturation kwenda kwenye ‘maximum’. Iwapo unaona mabadiliko yoyote ya rangi yasiyoendana nayo au ncha zozote za kidigitali kwenye picha hiyo, basi picha hiyo itakuwa ilifanyiwa mabadiliko fulani.

4. Tazama nyuma ya picha

Tazama vizuri vitu vinavyoonekana kwenye hiyo picha: angalia kwenye hiyo picha kama kuna magari, majengo, maandishi, nguo, mabango, watu, na kadhalika. Tazama kitu chochote hapo kinachoweza kukupa shaka juu ya usahihi na uhalisia wa picha hiyo. Thibitisha kuhusu hali ya hewa na mwanga wa jua wakati wa tukio husika.

5. Una uhakika kuwa hujawahi kuiona hiyo picha siku za nyuma?

Tafuta kwenye  Google Images na TinEye ili kuhakikisha kama picha hiyo iliwahi kutumika katika tukio linguine.

6. Ongeza uelewa wako kuhusu mitandao ya kijamii

Kila mtu au taasisi inayosambaza taarifa hufanya juhudi ya kuhakikisha watu wanayakubalia mawazo na fikra zake. Hakuna mtu asiyekuwa na upande anaouegemea katika utoaji wa taarifa zake. Kila mtu ana itikadi zake, na wakati fulani ukweli unaweza kupotoshwa kwa makusudi au hata kwa bahati mbaya.

Ili kuujua vizuri ulimwengu, tunahitaji kutafuta njia madhubuti za kuelewa jinzi mitandao ya kijamii inavyofanya kazi. Tunatakiwa kujifunza jinsi kile tunachokiona kinavyoweza kuwa sivyo kilivyo. Teknolojia ni nyenzo kubwa ya ugunduzi na kuudhibiti ukweli. Kabla ya kuihamisha taarifa au kubonyeza kitufe cha kuwaonesha watu kuwa waipenda, tafakari kwanza na ujiulize: “Je hii taarifa ninayotaka kuisambaza ni taarifa sahihi au nami ni sehemu ya utani wa mizaha ya mtandaoni  au kampeni ya upotoshaji wa taarifa?”


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment