MLIPUKO WA BOMU WAUA WATALII NCHINI MISRI


The site of a bomb explosion in the south Sinai resort town of Taba on February 16, 2014
Eneo ulipotokea mlipuko wa bomu katika mji wa Taba kusini mwa Sinai leo Februari 16, 2014.


Mlipuko mkubwa wa bomu katika eneo la Sinai nchini Misri, umewaua watu wasiopungua 5 wakiwemo watalii wanne kutoka Korea ya Kusini na kuwajeruhi wengine kadhaa.

Maafisa wa usalama katika eneo hilo wamesema kuwa watu hao walipoteza maisha baada ya bomu kulipuka ndani ya basi la watalii leo katika mji wa Taba kwenye Peninsula ya Sinai.

Mamlaka za eneo hilo zinasema kuwa watalii wanne kutoka Korea ya Kusini na dereva wa basi hilo walipoteza maisha papo hapo.

Kwa uchache watu 30 walijeruhiwa na kukimbizwa katika hospitali iliyokuwa eneo la jirani kwa matibabu.

"Kulikuwa na viungo vya miili na maiti. Niliiona maiti ya mtu mmoja aliyeonekana kuwa ni Mkorea, huku akiwa hana mguu,” alisema daktari anayeendesha kituo kimoja cha afya katika eneo hilo.

Siku za hivi karibuni eneo la Peninsula ya Sinai limekuwa likikumbwa na matukio mbalimbali, ambapo wanamngambo wamekuwa wakifanya mashambulizi dhidi ya vikosi vya usalama na kuyalenga maeneo mengine.

Kwa kawaida, Mabedui katika Peninsula hiyo wamekuwa wakiwateka wageni na kuwatumia nyenzo ya kuzungumza na mamlaka za serikali kutaka ziwaachie huru  ndugu zao waliofungwa.

Tukio la leo linakuja wakati makundi ya wanamgambo yakiwa yamedai kuhusika na mashambulizi na milipuko kadhaa tangu kuondolewa madarakani kwa Rais wa kwanza kuchaguliwa kidemokrasia nchini humo, Mohammed Mursi, aliyeondolewa na jeshi Julai 3, 2013.

Katika kulishughulikia suala hilo, serikali iliyowekwa madarakani na jeshi, ilianzisha operesheni maalumu, ikatuma vikosi vya askari wenye zana nzito za kijeshi katika eneo hilo.

Watu kadhaa wameshapoteza maisha wakati wa mapambano ya wanamgambo na jeshi la Misri katika eneo hilo la Sinai.

Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment