WAFARANSA WAWILI WAUAWA NCHINI MALI

French journalists Ghislaine Dupont (L) and Claude Verlon
Ghislaine Dupont (kushoto) na Claude Verlon 


WAANDISHI wawili raia wa Ufaransa wameuawa baada ya kutekwa na watu wenye silaha katika mji mmoja kaskazini mashariki mwa nchi ya Mali.

Taarifa iliyotolewa jana na Wizara ya Mambo ya Nje ya Ufaransa ilisema kuwa waandishi hao ambao walikuwa wakifanya kazi idhaa ya Radio France International (RFI), walikutwa na mauti katika nchi hiyo ya Afrika Magharibi.

"Waandishi wa habari wa RFI, Claude Verlon na Ghislaine Dupont walipatikana wakiwa wamekufa nchini Mali,” ilisema taarifa hiyo na kuongeza kuwa walitekwa na kundi lenye silaha katika mji wa Kidal.

"Serikali ya Ufaransa, kwa ushirikiano na mamlaka za Mali, itafanya kila juhudi kubaini mazingira ya vifo vyao mapema iwezekanavyo,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.

Mapema jana, duru kutoka kundi la waasi la National Movement for the Liberation of Azawad (MNLA), na vikosi vya usalama vya serikali ya Mali zilisema kuwa waandishi hao waliuawa katika viunga vya mji wa Kidal.

"Dakika kadhaa baada ya kuwafuatiliaji watekaji, tulitaarifiwa kuwa miili yao imepatikana ikiwa imepigwa risasi nje ya mji,” alisema kiongozi wa mji wa jirani wa  Tinzawaten, Paul-Marie Sidibe.

Chanzo kimoja kutoka ndani ya safu ya usalama wa serikali ya Mali kilisema kuwa wawili hao waliuawa karibu kilometa 12 (maili 8) nje ya mji, huku afisa mmoja mwandamizi wa waasi wa MNLA akisema pia kuwa miili hiyo ilikutwa nje ya mji wa Kidal.


Wawili hao walitekwa nyara baada ya kufanya mahojiano na mkazi mmoja wa Kidal, Ambeiry Ag Rhissa, aambaye ni afisa wa kundi la MNLA katika eneo hilo.


Aidha, shirika la RFI lilithibitisha habari hizo na kusema kuwa waandishi hao walipakiwa katika gari kabla ya kuwaua.

Idhaa hiyo imesema kuwa Verlon na Dupont walikuwa wamekwenda Kidal kwa mara ya pili, huku mara ya kwanza ikiwa ni mwezi Julai walipokwenda kuripoti kuhusu uchaguzi mkuu wa nchi hiyo.

Mara hii walikuwa wamekwenda kutengeneza ripoti ya matangazo maalumu yaliyokuwa yamepangwa kutangazwa Novemba 7, lakini sasa programu hiyo imefutwa.


Kufuatia tukio hilo, Rais wa Ufaransa, Francois Hollande alilaani mauaji hayo na kuyaita kuwa ni ya kinyama.


Ufaransa ilipeleka majeshi yake nchini Mali mnamo Januari 11, 2013 katika kile ilichokiita kuwa ni kuwazuia waasi wa nchi hiyo waliokuwa wakisonga mbele katika mapambano yao na kuhatarisha usalama wa Mali. 
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment