UTURUKI NA MISRI KATIKA MGOGORO MPYA WA KIDIPLOMASIA

 Turkey, Egypt expel ambassadors, downgrade diplomatic ties



Na Kabuga Kanyegeri, Istanbul

MISRI imemtaka balozi wa Uturuki kuondoka nchini humo na kuituhumu Ankara kuwa inaunga mkono makundi yanayoyumbisha uthabiti wa nchi, tuhuma ambazo zinaonekana kuelekezwa Uturuki kuwa inakiunga mkono chama cha rais aliyeondolewa madarakani, Muhammad Mursi.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Misri imesema kuwa balozi wa Uturuki nchini humo hatakiwi na kutaka aondoke kwa sababu ya kile ilichokielezea kuwa Uturuki imeendelea “kuingilia” mambo ya ndani ya Misri.

CHANZO CHA MGOGORO

Uturuki imekuwa mkosoaji mkubwa dhidi ya hatua hiyo ya kuondolewa kwa Mursi, na kukiita kitendo hicho kuwa ni “mapinduzi yasiyokubalika”.

Mwezi Agosti Uturuki na Misri ziliwaita mabalozi wao kwa muda baada ya Uturuki kushutumu vikali kitendo cha jeshi kumuondoa Mursi madarakani na operesheni kali iliyoongozwa na jeshi hilo kuyadhibiti maandamano ya kumuunga mkono Mursi. Baada ya hapo balozi wa Uturuki alirejea wiki mbili baadaye, lakini Misri iligoma kumrejesha balozi wake Ankara.

Chama cha Mursi cha Udugu wa Kiislamu, ambacho kimekuwa kikiitisha maandamano kikitaka Mursi arejeshwe madarakani, kinadaiwa kuwa na uhusiano wa karibu na chama tawala cha Uturuki cha Haki na Maendeleo (AKP).

UTURUKI YAJIBU MAPIGO

Uturuki imejibu mapigo ya Cairo kwa kutangaza kuwa balozi wa Misri ni mtu “asiyetakiwa” katika dalili mpya inayoashiria kukua kwa mgogoro baina ya mataifa hayo mawili yenye nguvu katika eneo la mashariki ya kati na ambao ni washirika wakubwa wa Marekani, mgogoro uliosababishwa na hatua ya jeshi la Misri kumuondoa madarakani aliyekuwa rais wa nchi hiyo, Muhammad Mursi mnano Julai 3 mwaka huu.

Wizara ya mambo ya Nje ya Uturuki, katika taarifa yake, imesema kuwa imesikitishwa na hali hiyo, lakini ikasema kuwa utawala wa mpito wa Misri utahukumiwa na historia kwa sababu uliingia madarakani kwa mazingira yasiyokuwa ya kawaida ya mapinduzi ya Julai 3.

Katika radiamali yake kwa msimamo wa Misri, Rais wa Uturuki, Abdullah Gül alizungumza kwenye televisheni ya taifa, TRT, na kusema kuwa: “Ninatumai uhusiano wetu utarejea katika hali yake ya kawaida.”

Rais Gül alielezea matarajio yake kuwa kipindi cha mgogoro huo wa kidiplomasia ni cha mpito na kwamba Uturuki inatarajia kuwa muda si mrefu Misri itarejea kuwa nchi ya kidemokrasia.

Mnamo Agosti 15, Waziri Mkuu wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan, alitoa wito wa kufanyika kikao cha dharura cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kujadili operesheni kali ya jeshi la Misri dhidi ya waandamanaji wanaomuunga mkono rais aliyepinduliwa, Muhammad Mursi.

Taifa hilo la Kiarabu liliangukia katika machafuko makubwa mwezi Julai baada ya jeshi kumuondoa madarakani rais wa kwanza kuchaguliwa kidemokrasia, bunge likavunjwa, matumizi ya katiba yakasitishwa, na kumtangaza mkuu wa Mahakama Kuu ya Katiba, Adly Mahmoud Mansour, kuwa rais wa mpito.

Serikali ya Mansour imeanzisha operesheni kali dhidi ya wafuasi wa Mursi na imewakamata wanachama 2,000 wa vuguvugu la udugu wa Kiislamu, akiwemo kiongozi mkuu wa vuguvugu hilo, Muhammad Badie.

Zaidi ya watu 1,000 waliaua ndani ya wiki moja katika ghasia baina ya wafuasi wa Mursi na vikosi vya usalama baada ya polisi kuzivunja kambi za waandamanaji katika operesheni kali ya Agosti 4.


Mauaji hayo yaliibua lawama ya kimataifa na kuzifanya taasisi mbalimbali za kimataifa kutoa wito wa kufanyika kwa uchunguzi huru kuhusu ghasia hizo.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment