ERDOĞAN: HATUTAWAHESHIMU WANAOINGIA MADARAKANI KWA NGUVU ZA KIJESHI






Na Kabuga Kanyegeri, Istanbul


WAZIRI Mkuu wa Uturuki, Recep Tayyip Erdoğan, ameendelea kushikilia msimamo wake wa kutoutambua utawala wa mpito wa Misri akisema kuwa haukuchaguliwa na wananchi.

Akizungumza katika jimbo la Trabzon kwenye pwani ya Bahari Nyeusi, Erdoğan alisisitiza msimamo wake kuwa kamwe hatawaheshimu wale wanaongia madarakani kwa mapinduzi ya kijeshi.

"Tuko upande wa wananchi wa Misri wanaodhulumiwa. Tuko upande wa wale waliokuwa katika medani ya Rabaa al-Adawiya," alisema, akiwakusudia wale walioandamana katika uwanja wa Rabia mjini Cairo kupinga hatua ya jeshi la nchi hiyo kumuondoa madarakani rais Muhammad Mursi.

Katika kuonesha msimamo wake ambao amekuwa nao tangu mapinduzi hayo, alinyosha juu mkono wake akiwa amevikunjua vidole vinne ambavyo hutumika kama ishara ya wale wanaopinga mapinduzi hayo nchi Misri.

“Hatukuwahi kuwaheshimu wale waliofanya mapinduzi na kamwe hatutafanya hivyo. Tutaendelea kuheshimu matakwa ya wananchi, hapa kwetu na popote pale duniani. Ndio maana msimamo wetu upo wazi na tupo makini sana na suala hili.”

Aidha, Erdoğan amekosoa vikali hatua ya jeshi kuingilia siasa akielezea kuwa jeshi linapaswa kukaa nje ya siasa na kuangalia majukumu yake.


Uhusiano wa kidiplomasia umeingia katika sura mpya baada ya hapo jana Misri kumfukuza balozi wa Uturuki nchini humo kwa kile ilichoeleza kuwa Ankara imeendelea kuingilia mambo ya ndani ya nchi hiyo kwa kuyaunga mkono makundi iliyoyaelezea kuwa yanayumbisha uthabiti wa nchi, yaani vuguvugu la Udugu wa Kiislamu. Uturuki ilijibu mapigo kwa kumfukuza balozi wa Misri nchini humo.

Uturuki imekuwa mkosoaji mkubwa wa watawala wa Misri na msimamo wa Erdoğan umekubwa mwiba kwa utawala wa Cairo, ambao unajaribu kutuliza hali ya mambo iliyofuatia kuondolewa madarakani kwa rais aliyechaguliwa na wananchi, Muhammad Mursi, ambapo jeshi lilimchagua mkuu wa mahakama ya katiba, Adly Mahmoud Mansour kuwa rais wa mpito, likavunja bunge na kusimamisha matumizi ya katiba.


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment