AJIPIGA RISASI AKISHINIKIZA KURUDIANA NA MTALAKA

 
Kamanda wa Polisi Tabora, Peter Ouma




MFANYABIASHARA maarufu mjini Tabora, Hakimu Hamdun, mkazi wa Kata ya Kanyenye anashikiliwa na Polisi akituhumiwa kujaribu kujiua kwa kujipiga risasi kutokana na wivu wa mapenzi.

Kamanda wa Polisi mkoani Tabora, Kamishna Msaidizi Peter Ouma, alisema jana kuwa Hamdun alijaribu kujiua kwa risasi wiki iliyopita saa kumi na mbili jioni nyumbani kwake eneo la Kanyenye mjini Tabora.

Alisema kuwa Hamdun ambaye kwa sasa amelazwa katika Hospitali ya Mkoa Kitete kwa matibabu, alijipiga risasi baada ya mkewe aliyempa talaka mbili, kumtaka afuate utaratibu wa ndoa ili warudiane.

Inadaiwa Hamdun alimpa talaka mbili mtalaka huyo, Joha Binti Sudi, lakini baadaye alibadilisha mawazo na kumtaka warudiane huku akimtishia kumuua kama asipokubali.

Kwa mujibu wa madai ya Kamanda Ouma, wanandoa hao waliotalikiana walikuwa wakiishi nyumba tofauti na Hamdun aliamua kumfuata mwanamke alipokuwa akiishi akiwa na gari lake na kumtaka warudiane.

Hata hivyo, alidai mwanamke huyo alikataa kurudiana kiholela na kumtaka Hamdun kama kweli anampenda, afuate utaratibu wa Dini ya Kiislamu ndipo watimize azma yao hiyo ya kurudiana.

KUJIUA
Badala ya kufuata utaratibu, inadaiawa hamdun alienda kwenye gari lake na kuchukua bunduki aina ya Shot gun na kwenda nyumbani kwake ambapo alifunga milango, akajipiga risasi katika ubavu wa kushoto.

Kwa mujibu wa Kamanda Ouma, mtuhumiwa huyo hali yake inaendelea vizuri lakini amepoteza sifa ya kumiliki bunduki na hivyo hatapewa tena.

Aidha, Hamdun atakapomaliza matibabu atafikishwa mahakamani kujibu mashitaka yake ikiwemo ya kutishia kuua na jaribio la kutaka kujiua.


CHANZO: Habari Leo
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment