KIONGOZI MWANDAMIZI WA ‘MUSLIM BROTHERHOOD’ AKAMATWA


Essam El-Erian (file photo)
Essam el-Erian



Na Kabuga Kanyegeri


VIKOSI vya usalama nchini Misri vimemkamata kiongozi mwandamizi wa vuguvugu la Udugu wa Kiislamu, Essam el-Erian, katika muendelezo wa kulidhibiti vuguvugu hilo.

Kwa mujibu wa Wizara ya Mambo ya ndani ya nchi hiyo, Erian ambaye ni naibu kiongozi wa chama cha Uhuru na Uadilifu kilicho chini ya vuguvugu hilo, amekamatwa leo baada ya Kikosi Maalumu kuivamia nyumba yake.

Amekamatwa kufuatia amri iliyotolewa na mwendesha mashitaka wa serikali, ambaye alimtuhumu kwa “kuchochea ghasia” na “kusaidia vitendo vya kihalifu.”

Erian ndiye kiongozi pekee wa ngazi ya juu wa vuguvugu hilo ambaye alikuwa hajakamatwa baada ya viongozi wengine wote wa kundi hilo kutiwa nguvuni.

Idadi kubwa ya maafisa wa vuguvugu la Udugu wa Kiislamu wamewekwa korokoroni na vikosi vya jeshi na polisi tangu kuondolewa madarakani kwa aliyekuwa rais wa nchi hiyo Muhammad Mursi mapema mwezi Julai.

Mnamo Julai 3, mkuu wa jeshi la Misri, Jenerali Abdulfattah al-Sisi alitangaza kuwa Mursi alikuwa ameondolewa madarakani baada ya “jeshi kumpiindua.” Vilevile al-Sisi alisitisha matumizi ya katiba na kulivunja bunge.

Mwezi Septemba, mahakama moja nchini humo ililipiga marufuku vuguvugu la Udugu wa Kiislamu kufanya kazi kama taasisi isiyokuwa ya kiserikali (N.G.O) na kuamuru mali zake zote zitaifishwe.

Katika wimbi jingine la kulibana vuguvugu hilo, mwezi Agosti, kwa uchache watu 1,000, wengi wao wakiwa wafuasi wa Mursi, waliuawa na wanachama wengine wa vuguvugu hilo wapatao 2,000 wakakamatwa, baada ya serikali ya mpito iliyoteuliwa na jeshi kuamuru kuyasambaratisha maandamano ya kumuunga mkono Mursi.

Vuguvugu hilo kongwe liliunda chama cha kisiasa mwaka 2011, miezi kadhaa baada ya kuanguka kwa rais wa zamani, Husni Mubarak.


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment