RAIS WA GAMBIA: SING’ATUKI MADARAKANI

Gambian President Yahya Jammeh (File photo by Reuters)
Rais wa Gambia Yahya Jammeh 


Rais Yahya Jammeh wa Gambia ametangaza wazi kuwa hatong’atuka madarakani licha ya kushindwa na kiongozi wa upinzani Adama Barrow kwenye uchaguzi wa urais uliofanyika mapema mwezi huu.

Katika maelezo yake kwenye televisheni ya serikali, pamoja na mambo mengine alilaani hatua ya usuluhishi inayofanywa na viongozi wa Jumuiya ya Kiuchumi ya mataifa ya Afrika Magharibi (ECOWAS), ambao wamekuwa wakijaribu kumshawishi akabidhi madaraka kwa amani wakati muda wake utakapomalizika tarehe 18 Januari.

“Mimi sio mwoga. Haki yangu haiwezi kuzimwa na kukiukwa. Huu ni wadhifa wangu. Hakuna anayeweza kuninyima ushindi isipokuwa Mwenyezi Mungu,” alisema rais huyo ambaye amekuwa akidai kuwa uchaguzi ulikuwa na kasoro nyingi.

Awali Jammeh aliyakubali matokeo ya uchaguzi huo uliofanyika Desemba 1, ambapo Barrow alitangazwa kuwa mshindi, lakini alitengua kauli yake wiki moja baadaye na kutaka uchaguzi urudiwe.

Hatua yake ya kuyakataa matokeo iliibua wasiwasi katika taifa hilo na kusababisha jumuiya ya kimataifa kumshinikiza ayakubali matokeo na kung’atuka madarakani. Wiki iliyopita ECOWAS ilisema kuwa Jammeh anapaswa kuondoka madarakani mwezi ujao na kuahidi kuchukua hatua zote za lazima kuhakikisha  matokeo ya uchaguzi huo yanaheshimiwa.



Hata hivyo, katika kauli yake ya jana, Jammeh alisema kuwa mikutano yake na wasuluhishi wa ECOWAS ilikuwa ya “utaratibu tu” na kwamba hatong’atuka.

Uamuzi wake huu unatarajiwa kuibua mivutano zaidi katika nchi hiyo ambapo jeshi limeshawekwa tayari huku likiwa limeyadhibiti makao makuu ya tume ya uchaguzi katika hatua ambayo inaelezwa kuwa rais huyo anajaribu kuonesha misuli yake.


Kiongozi wa upinzani nchini Gambia Adama Barrow (katikati) baada ya kutangazwa mshindi wa uchaguzi Desemba  2, 2016 

Naye msemaji wa upinzani, Halifa Sallah, jana alisema kuwa Jammmeh hatoshitakiwa kwa kuyakataa matokeo kama atafanya uamuzi wa kukabidhi madaraka kwa amani.

“Rais mteule Barrow anasema kuwa ataamiliana na rais Yahya Jammeh kama kiongozi mstaafu wa nchi na atakuwa akichukua ushauri wake,” Sallah alisema. Alisema kuwa Jammeh hana mamlaka ya kikatiba ya kubaki madarakani baada ya mwezi Januari, huku akionya kuwa rais yeyote anayepoteza uhalali wa kikatiba anakuwa muasi.

Marekani, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na mashirika ya kimataifa yametoa wito wa makabidhiano ya madaraka kwa amani.

Rais Francois Hollande wa Ufaransa ambayo ilikuwa koloni lake, amesema kuwa matokeo ya uchaguzi hayakuwa na shaka yoyote na kwamba Barrow anatakiwa kuapishwa mapema iwezekanavyo.


Jammeh aliingia madarakani kwa mapinduzi ya kijeshi mwaka 1994 na amekuwa mamlakani tangu wakati huo. 
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment