CHAMA TAWALA CHASHINDA UCHAGUZI IVORY COAST

Ivory Coast: Ruling coalition wins elections
Rais Alassane Ouattara wa Ivory Coast



ABIDJAN, Ivory Coast

Muungano unaotawala nchini Ivory Coast umeshinda uchaguzi na kunyakua viti 167 vya ubunge kati ya viti 255.

Matokeo hayo yamethibitishwa na tume ya uchaguzi ya nchi hiyo jana jioni.

Akizungumza na waandishi wa habari, mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi, Youssouf Bakayoko, amesema kuwa chama cha Watetezi wa Demkrasia na Amani (RHDP) kilichukua nafasi ya kwanza kwa kupata asilimia 65.7 ya viti kikifuatiwa na wagombea huru waliopata asilimia 29.

Muungano wa Demokrasia na Amani nchini Ivory Coast kimechukua nafasi ya tatu kikiwa na viti sita (asilimia 2.36). Chama cha Rais wa zamani wa nchi hiyo, Laurent Gbagbo cha FPI, kilipata viti vitatu.

"Tuna wabunge 254 waliochaguliwa, wanaojumuisha wanaume 225 na wanawake 29," alisema Bakayoko.

Upigaji kura wa jimbo lililobaki utafanyika ndani ya siku 15 katika wilaya ya Guiglo magharibi mwa nchi hiyo. Mchuano utakuwa kati ya mgombea huru na yule wa RHDP.

Mwezi jana wapiga kura walipiga kura kwa wingi kupitisha katiba mpya ambayo inampa fursa Rais Alassane Ouattara kugombea muhula wa tatu.


Ouattara aliyeingia madarakani mwaka 2010 alichaguliwa tena kwa muhula wa pili mwezi Oktoba mwaka 2015.

Ivory Coast ilitumbukia katika ghasia za baada ya uchaguzi wa mwaka 2010 ambazo zilisababisha vifo vya watu wasiopungua 3,000.

Rais wa wakati huo, Gbagbo alikataa kuyakubali matokeo ya uchaguzi, na wafuasi wake walidai kuwa Ouattara hakuwa raia halisi wa nchi hiyo.

Gbagbo, ambaye alitawala kati ya mwaka 2000 na 2010, kwa sasa anashikiliwa na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu iliyo mjini Hague, akishitakiwa kutenda uhalifu dhidi ya binadamu.


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment