WATU 48 WAUAWA KATIKA SHAMBULIZI NCHINI KENYA

Lamu 


WATU 48 waliuawa baada ya watu wenye silaha kushambulia mji wa Mpeketoni, Kaunti ya Lamu usiku wa kuamkia leo katika pwani ya Kenya.

Shambulio hilo lilitekelezwa na washambulizi 50 waliokuwa wamejihami kwa silaha nzito kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na serikali leo.

Shirika la Msalaba Mwekundu limesema idadi ya waliofariki ni 48, ingawa polisi walikuwa wamethibitisha vifo vya 26 pekee.

Katibu Mkuu wa shirika hilo Abbas Gullet alisema wawili walijeruhiwa na wanatibiwa katika hospitali iliyo karibu.

“Tumekusanya miili 26 ambayo tumepeleka katika chumba cha kuhifadhia maiti. Tunaendelea kusaka miili zaidi,” Bw Benso Maisoti ambaye ni Kaimu Kamishna wa Wilaya aliliambia shirika la AFP.

Hata hivyo imeripotiwa leo asubuhi kuwa mji wa Mpeketoni ambao mashambulizi yalifanyika uko katika hali ya utulivu.

Washambuliaji hao walitekeleza tendo hilo kutoka kwenye magari mawili ya usafiri pamoja na kuchoma moto hoteli mbili, kwa mujibu wa ripoti ya maafisa wa serikali. Kwa mujibu wa maafisa hao wengi wa waathiriwa walipigwa risasi vichwani.

Mlinzi wa Kamishna wa Lamu Bw Leonard Omollo alikuwa miongoni mwa watu waliouawa.

Maafisa wameongeza kusema kuwa miili 13 ilipatikana katika makao ya Mama Ngina na mingine Saba kutoka kwa Hoteli ya Capital.

Miili mingine miwili ilipatikana katika Jumba la Wageni la Breeze View huku miili zaidi ikiwa imetapakaa kote mjini.

Msemaji wa Polisi Zipporah Mboroki awali alikuwa amesema walikuwa wamepata miili 14 ingawa idadi hiyo ilitarajiwa kuwa zaidi.

Washambuliaji hao vile vile walivunja benki tatu ambazo ni Kenya Commercial Bank, Equity na Cooperative. Hata hivyo haijabainika ikiwa waliiba pesa au la.

SERIKALI YA KENYA YAKOSOLEWA

Chama cha ODM kiliomboleza waliouawa Mpeketoni, Lamu na kusema ni jukumu la Serikali ya Kitaifa kuhakikisha usalama wa raia popote nchini humo.

Katibu Mkuu wa chama hicho Prof Anyang' Nyong'o kupitia taarifa aliitaka Serikali ichukue hatua upesi kudhibiti hali Lamu na maeneo mengine ya nchi yaliyo hatarini.

Baadhi ya watu walitoa wito kwa Rais Kenyatta kuwafuta kazi wakuu wa usalama.


“Mheshimiwa Uhuru lazima afanyie mabadiliko baraza lake la mawaziri na awastaafishe wakuu wake wa usalama upesi kwa maslahi ya taifa,”  alisema wakili mashuhuri Ahmednasir Abdullahi kupitia Twitter.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment