SHEIKH MWINGINE AUAWA NCHINI KENYA

 


Watu wasiojulikana wamemuua kwa kumpiga risasi Mwenyekiti wa Maimamu na Wahubiri wa Kiislamu nchini Kenya, Sheikh Mohammed Idris, asubuhi ya leo katika eneo la Likoni, Mombasa.

Aidha, Sheikh Mohammed alikuwa mwenyekiti wa Masjid Sakina mjini Mombasa ambao hivi karibuni ulidaiwa kuingia katika mzozo na baadhi ya vijana ambao alikuwa akiwaona kuwa wenye msimamo mkali.

Polisi wanasema mwili wa marehemu ulipelekwa kwenye chumba cha kuhifadhia maiti katika hospitali ya Pandya.

Aidha, Polisi wanasema kuwa muuaji bado hajajulikana na kwamba Sheikh aliuawa karibu na nyumbani kwake wakati akitoka msikitini. Kwa muda sasa Sheikh Mohammed Idris alikuwa akielezea hofu yake ya kuuawa baada ya kupewa vitisho mara kadhaa kutoka kwa vijana hao.

Mkuu wa upelelezi mjini Mombasa Henry Ondieki anasema kuwa wanashuku kwamba Sheikh Idris ameuawa na mtu anayemjua vizuri na kwamba walimfuatilia kwa muda mrefu kabla ya kumshambulia.

Taarifa za ndani zinadai kuwa Sheikh Idris alikuwa mkosoaji mkubwa wa baadhi ya makundi ya vijana aliyoyatazama kama makundi yenye msimamo mkali na kuwataka polisi kuwashughulikia wale aliodhani wanahusika na kuwatia kasumba vijana hao kwa madai kuwa walikuwa wakisababisha ghasia kwa jina la Uislamu. Msimamo wake huo uliwakasirisha vijana wengi waliomuona kama msaliti.



Katika miezi ya hivi karibuni, mji wa Mombasa ambao ni mji wa pili kwa ukubwa na kitovu cha utalii nchini Kenya, ni miongoni mwa miji kadhaa ambayo imekuwa ikikumbwa na ghasia mbalimbali huku viongozi kadhaa wa kidini wakiuawa.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment