MWANAMUME mmoja huko Kenya aliyepatikana na hatia ya
kumpiga mkewe na kumuumiza kwa madai kuwa alichelewa kumpa chakula cha mchana,
amehukumiwa kwenda jela miezi mitatu ama alipe faini ya Sh5, 000 za Kenya.
Mahakama ya Eldoret nchini humo ilimpata Gideon Kenneth
Gavana na hatia ya kumpiga mkewe na kumwacha na majeraha mabaya ya kichwa,
miguu na mikono.
Hakimu Msimamizi mkuu Bw Samwel Mokua alitoa uamuzi huo
baada ya Bi Sophia Gavana na wanawe wawili kutoa ushahidi mahakamani kuhusiana
na kilichotokea siku hiyo.
Mahakama ilielezwa kuwa, mshtakiwa aliwasili nyumbani
kwake katika eneo la Road Block mojawapo ya viungani mwa mji wa Eldoret mnamo
Mei 24 mwendo wa saa saba mchana na kumkuta mkewe jikoni akiwa anaanda chakula
cha mchana.
Bw Gavana alisemekana kuitisha chakula kwa njia isiyo ya
kawaida na hata baada ya kuambiwa na mkewe kuwa asubiri, alikataa kata kata na
kuongea kwa sauti ya juu kana kwamba alikuwa amenyimwa chakula hicho.
“Nilipomletea mume wangu chakula, alikuwa amekasirika na
akataka nibadilishe sahani na nimwekee chakula kwenye sahani nyingine ambayo
alisema aliipenda sana.
Nilipokuwa narudi ndani ya nyumba kuitafuta ile sahani,
mume wangu alinishika kwa nyuma na kuniangusha chini kabla ya kuanza kunipiga
kwa ngumi na mateke na hadi wanangu wawili walipoingilia kati na kuniokoa,”
Sophia alisema.
Barua kutoka kwa daktari wa hospitali ya eneo hilo la
Baharini Bonface Watila Ndula ilionyesha kuwa, ni kweli mlalamikaji alifikishwa
katika kituo hicho cha afya akiwa na maumivu mabaya ya kichwa na sehemu
nyingine za mwili.
CHANZO: Swahilihub.com
0 comments:
Post a Comment