KOCHA IVORY COAST AJIUZULU
Mwalimu wa timu ya soka ya Ivory Coast Sabri Lamouchi amejiuzulu kuifundisha timu hiyo baada kushindwa kufuzu kwa hatua ya 16 bora katika michuano ya Kombe la Dunia.
Tembo hao wa magharibi mwa Afrika walikubali kichapo cha 2-1 kutoka kwa Ugiriki katika mchezo wao wa mwisho wa Kundi C usiku wa kuamkia leo, matokeo yaliyowafanya kushika nafasi ya tatu huku wapinzani wao wakishika nafasi ya pili.
Mkataba wa Lamouchi ulitakiwa kufikia kikomo baada ya tamati ya Kombe la Dunia.
"Nimesikitishwa sana na wachezaji," alisema kocha huyo mwenye umri wa miaka 42.
Matokeo ya sare yangetosha kuifanya Ivory Coast kushika nafasi ya pili na hivyo kuungana na Colombia katika hatua ya 16 bora.
Ndoto yao ilikaribia kutimia kabla ya Georgios Samaras kupata penalti yenye utata na kuivusha Ugiriki.
"Ivory Coast ni taifa kubwa katika soka na huu ulikuwa mchezo muhimu, muhimu sana," alilalama Lamouchi.
"Baada ya kazi kubwa na kujitoa mhanga, sisi sote na kila mtu nchini Ivory Coast amehuzunika sana."
Lamouchi, kiungo wa zamani wa klabu za Auxerre na Monaco ambaye pia aliwahi kuzichezea klabu za Parma na Inter Milan za Italia, aliteuliwa kuwa kocha mkuu wa Ivory Coast Mei 2012 ikiwa ni kazi yake ya kwanza kama meneja.
Alipewa jukumu hilo walipofika hatua ya robo fainali ya michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika.
0 comments:
Post a Comment