JAJI ALIYEMHUKUMU KIFO SADDAM HUSSEIN AUAWA


Jaji aliyemhukumu adhabu ya kifo kiongozi wa zamani wa Iraq Saddam Hussein amekamatwa na kuuawa na wapiganaji wa kundi la Dola ya Kiislamu katika Iraq na Sham (ISIS), imeelezwa.

Raouf Abdul Rahman, ambaye aliagiza Saddam anyongwe mwaka 2006, ameripotiwa kuuawa na waasi kama kisasi kwa kifo cha Saddam aliyenyongwa akiwa na umri wa miaka 69.

Kifo chake hakijathibitishwa na serikali ya Iraq, lakini maofisa hawakukanusha taarifa zilizopatikana wiki iliyopita kwamba alikuwa ametekwa. Inaaminika alikamatwa Juni 16 na kisha kuuawa siku mbili baadae.

Mbunge kutoka Jordan, Khalil Attieh, ameandika katika ukurasa wake wa Facebook kuwa Jaji Rahman, aliyeongoza Mahakama Maalumu wakati wa kesi ya Saddam, alitekwa na kuuawa.


“Wanamapinduzi wa Iraq walimkamata na kumuua katika kulipiza kisasi kwa kifo cha marehemu Saddam Hussein,” aliandika, kama alivyonukuliwa na mtandao wa Al-Mesyroon.

Aidha, Attieh alisema kuwa Jaji Rahman alijaribu kutoroka kutoka bila mafanikio.

Vile vile ukurasa wa Facebook wa Izzat Ibrahim al-Douri, ambaye alikuwa msaidizi wa  Saddam na ambaye katika siku za hivi karibuni amekuwa na ushawishi mkubwa miongozi mwa waasi, aliandika kuwa waasi hao walikuwa wamemkamata Jaji Rahman.

Jaji Rahmann, ambaye alizaliwa katika mji wa Kikurd wa Halabja, alichaguliwa kuongoza kesi hiyo mwezi Januari 2006 baada ya jaji wa mwanzo Rizgar Amin kukosolewa kuwa alikuwa laini sana katika kumshughulikia Saddam na washitakiwa wenzake.


Jaji huyo mwenye watoto watatu alihitimu masomo yake katika shule ya sheria ya Chuo Kikuu cha Baghdad mwaka 1963 na kufanya kazi kama mwanasheria kabla ya kuteuliwa kuwa jaji mkuu wa mahakama ya rufaa ya Kurdistan mwaka  1996.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment