OBAMA: URUSI ITAUMIA ZAIDI




Rais wa Marekani Barack Obama kwa mara nyingine ameionya Urusi kuhusu mgogoro wa Ukraine akisema kuwa Moscow inaweza kukabiliwa na maumivu zaidi kama hakutakuwepo na hatua madhubuti ya kuzuia hali ya mdororo na machafuko inayoendelea katika taifa hilo lililokuwa sehemu ya Muungano wa Usovieti.

Ikulu ya Marekani imesema kuwa Obama alitoa onyo hilo wakati akizungumza kwa njia ya simu na Rais wa Urusi Vladimir Putin jana Jumatatu.

"Rais amezungumza na Rais Putin na kwa mara nyingine amemtaka kuunga mkono amani badala ya kuruhusu usambazaji wa silaha na zana kwenye mpaka na kusaidia waasi na wanaotaka kujitenga ambao wanaendelea kuvuruga hali ya mambo nchini Ukraine,” msemaji wa Ikulu ya Marekani Josh Earnest aliwaambia waandishi wa habari.

"Urusi itakabiliwa na gharama zaidi iwapo hatutoona hatua madhubuti za kutuliza hali ya mambo,” alinukuu ujumbe wa Obama kwa Putin.

Wakati huohuo, Ikulu ya Urusi Kremlin imetoa taarifa ikisema kuwa viongozi hao walijadili juu ya njia za kukomesha mzozo huo ambapo Putin alisisitiza juu ya umuhimu wa kusimamisha mapigano nchini Ukaraine na kuanzisha mazungumzo baina ya pande zinazozozana.

"Walijadili utekelezaji wa mpango wa amani uliopendekezwa na Rais Petro Poroshenko (wa Ukraine)," ilisema taarifa ya Kremlin. "Putin alisisitiza kwamba kipaumbele kinatakiwa kutolewa kwenye suala la kusitisha operesheni za kijeshi na kuanza mazungumzo ya moja kwa moja baina ya pande kinzani.”

Kiongozi huyo wa Urusi pia aliashiria juu ya masuala ya kibinadamu, ikiwemo haja ya dharura ya kuwapelekea msaada raia walaioathiriwa na mapigano mashariki mwa Ukraine.

Aidha, walijadili masuala ya kimataifa kama vila kadhia ya Iraq, Syria, na programu ya nyuklia ya Iran.

Marekani na Urusi zimekuwa katika mzozo kuhusu eneo la Crimea, ambapo Washington inaituhumu Moscow kuwa ilikuwa nyuma ya “kura haramu ya maoni ya kujiondoa kwa Crimea” kutoka Ukraine na kuchochea machafuko mashariki mwa nchi hiyo.


Moscow imeyakanusha madai hayo kwa kuyaita “yasiyokuwa na maana” na kukana moja kwa moja kuhusika kwa vikosi maalumu vya Urusi kuchochea ghasia nchini Ukraine.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment