NGASA ALIPA MAMILIONI YA SIMBA

 



HATIMAYE mshambuliaji wa Yanga, Mrisho Ngasa, amelipa faini ya sh milioni 45 kama alivyokuwa ameadhibiwa na Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), baada ya kuwekewa pingamizi la usajili ya klabu ya Simba.

Simba ilipinga Ngasa kusajiliwa na Yanga kwa madai ina mkataba naye walioingia wakati wakimsajili kwa mkopo kutoka Azam FC msimu uliopita, ambapo Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji chini ya Mwenyekiti wake, Alex Mgongolwa, ilimhukumu mchezaji huyo kutocheza mechi sita na kulipa sh milioni 30 alizokuwa amechukua kwa Wekundu wa Msimbazi na riba asilimia 50, ndipo aweze kurejea dimbani.

Kutokana na kulipa fedha hizo, Ngasa anatarajiwa kushuka dimbani leo kuwavaa Ruvu Shooting katika mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Majira ya saa 9 alasiri jana, Ngasa aliwasili makao makuu ya TFF Karume Ilala, akiwa amebeba begi jeusi lenye hundi ya fedha hizo, akisindikizwa na watu watatu akiwemo mjumbe wa sekretarieti ya Yanga, Mkenya Patrick Naggi.

Mara baada ya kukabidhi hundi hiyo katika ofisi ya fedha ya shirikisho hilo, Ngasa alisema ameamua kulipa fedha hizo ili aweze kuitumikia klabu yake ya Yanga katika mchezo wa leo, kwani anaumizwa na matokeo ambayo timu yake inayavuna kwa sasa.

Aidha Ngasa aliwataka wachezaji wenzake kutofanya ambayo yeye kayafanya na kuwashauri kutafuta wanasheria ambao watakuwa wakisimamia haki zao.

Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah, alisema jana kuwa kuanzia msimu huu kila mchezaji mwenye mkataba na klabu yake, ametengenezewa leseni ambayo itakuwa ikionyesha kuanza kwa mkataba na kumalizika kwake.

Osiah alisema wameamua kufanya hivyo baada ya kuona hodi zinazidi TFF kwa wachezaji kuulizia mikataba yao na kusababisha usumbufu usio wa lazima, hivyo kwa utaratibu huo watakuwa wamefanikiwa kuuepusha.

Akizungumzia mchezo wa leo, Kocha Mkuu wa Yanga, Ernie Brandts, alisema kuwa yuko tayari kumtumia mchezaji huyo kwa kuwa ni kati ya anaowahitaji katika kikosi chake na alitamani kufanya hivyo siku zilizopita ila ilishindikana kutokana na adhabu hiyo.

Brandts alisema mchezo wa leo ana imani kubwa timu yake itaibuka na ushindi, kutokana na marekebisho aliyoyafanya mara baada ya kukubali kichapo cha mabao 3-2 kutoka kwa Azam FC Jumamosi iliyopita.

Mbali na mchezo huo unaotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa, mechi nyingine ni kati ya Rhino Rangers na Kagera Sugar dimba la Ali Hassan Mwinyi Tabora huku Mbeya City wakiwakaribisha Coastal Union uwanja wa Sokoine na Mgambo JKT watakuwa wenyeji wa ndugu zao JKT Oljoro kwenye uwanja wa Mkwakwani Tanga.


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment