MAKACHERO WABAINI GARI WALILOTUMIA AL-SHABAAB





MAKACHERO wa kimataifa kwa kushirikiana na wale wa Kenya, wamesema kuwa wamepata gari wanaloamini lilitumiwa na kundi la kigaidi la Al-Shabaab wakati walipofanya shambulizi katika jengo la kibiashara la Westgate jijini hapa na kuua watu zaidi ya 67.

Taarifa hizo zimetolewa na mmoja wa maofisa ambaye hakupenda kutaja jina lake kwa sababu ya kutovuruga uchunguzi wao, akisema kuwa njia wanayotumia ni kufuatilia wamiliki wa magari wanayoyakuta nje ya jengo hilo.

Aliongeza kuwa kwa sasa bado wanaendelea kuyatazama magari mengine ambayo yapo nje ili kuyagundua zaidi yalivyotumiwa na washambuliaji.

Katika taarifa nyingine zilizotolewa na Muungano wa Waandishi wa Habari, zimeeleza kuwa wanahabari wao waliwashuhudia makundi ya wachunguzi wa Kenya na wale wa kigeni wakiwa wanalichunguza gari hilo aina ya Saloon lenye rangi ya fedha, lililokuwa imeegeshwa mita 20 kutoka kwenye lango la kuingilia kwenye jengo hilo.

Walisema kuwa gari hilo lilikuwa limefunguliwa mlango wake, huku wachunguzi hao wakiwa wanalipiga picha ikiwa ni pamoja na kuandika, lakini waligoma kuzungumzia kile walichokiona.

Polisi wa nchini Kenya wamekuwa hawatoi taarifa kwa kina tangu washambuliaji hao walipotoa vitisho kwa mataifa ya Afrika Mashariki.

Kwa mujibu wa Waziri wa Usalama wa Ndani, Joseph ole Lenku, uchunguzi huu utachukua muda wa wiki moja kuhakikisha wanaopoa miili ya watu ambao wamefukiwa kwenye jengo hilo kama wapo.

Kundi la Al-Qaeda linalofungamana na Al-Shabaab limetoa vitisho vya kuwepo kwa shambulio jingine kutokana na Serikali ya Kenya kupeleka vikosi vyake kuishambulia Al-Shabaab nchini Somalia.

Kazi ya kutafuta wahalifu wa tukio hilo inafanywa na mawakala wa FBI kutoka Marekani, vikosi vya usalama vya Uingereza, Canada na Ujerumani.

Pamoja na uchunguzi huo, pia taarifa kutoka ndani ya Jeshi la Kenya zimeeleza kuwa kuna uwezekano mkubwa wa washambuliaji wa tukio hilo kukimbia siku waliyokuwa wamefanya tukio hilo.

Kikosi cha Msalaba Mwekundu kinasema kuwa watu 61 hawajulikani waliko.

Lakini idadi ya watu waliofariki imebaki kuwa kitendawili kutokana na serikali kusema ni 67 huku vikosi vya Al-Shabaab vikisema ni zaidi ya 177.

Katika hatua nyingine, Serikali ya Kenya imesema kuwa shambulio la kigaidi halijaathiri mipango yake ya kuongeza karibu dola bilioni 1.5 kwenye makubaliano yao ya ubia wa kimataifa.

Kenya inatafuta nafasi kubwa katika masoko ya kimataifa ili kufufua miundombinu ya tangu kipindi cha ukoloni ambayo kwa sasa imeharibika na kuongeza kasi ya uchumi ambao umeporomoka.

Mpango huo wa ubia wa kimataifa ambao utakuwa wa kwanza mkubwa katika taifa hilo la ukanda wa jangwa la Sahara, umepangwa kufanyika baadaye Novemba mwaka huu.

Katibu wa Hazina, Henry Rotich alisema kuwa uchumi wa Kenya kama ilivyo ari ya watu wake, haujatikiswa na janga hilo la hivi karibuni.


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment