MBOWE: YAPENI NAFASI MAZUNGUMZO SUALA LA EAC

 


KIONGOZI  kambi rasmi ya Upinzani Bungeni, Mh. Freeman Mbowe, ametahadharisha dhidi ya wanasiasa wanaoitaka serikali kujiondoa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Akizungumza katika Mkutano wa 13 wa Bunge unaojadili Mpango wa Taifa wa Maendeleo ya Kiuchumi kwa mwaka 2014/2015, Mheshimiwa Mbowe alitahadharisha kuwa hatua ya kujitoa EAC itakuwa na athari mbaya kwa wananchi.

Aidha, siku ya Jumanne, Mh. Mbowe aliwatahadharisha baadhi ya wanasiasa ambao wamekuwa wakitoa kile alichokiita kuwa ni maneno makali dhidi ya mataifa mengine wanachama wa EAC.

Mapema Jumatano, baadhi ya Wabunge waliishinikiza serikali ijitoe EAC au ifanye mpango wa kuunda jumuiya nyingine kwa kuzishirikisha nchi nyingine au Tanzania iache kujihusisha na shughuli za kikanda.

Wabunge walielezea wasiwasi wao juu ya ‘muungano wa hiari’ ulioundwa na Kenya, Uganda na Rwanda, ambao walisema kuwa wanajihusisha na shughuli na mazungumzo mbalimbali bila kuzihusisha nchi za Tanzania na Burundi.

Kwa mujibu wa Wabunge hao, mataifa hayo matatu yamekuwa yakizungumzia itifaki na mpango wa kuharakisha uundwaji wa shirikisho la kisiasa.

Mbunge wa Same Mashariki (CCM), Anne Kilango Malecela alisema kuwa itakuwa bora kama Tanzania itaacha kujihusisha kabisa na masuala yanayoihusu Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Naye mbunge wa viti maalumu (CUF) Bi Rukia Ahmed, aliitaka serikali kupeleka muswada bungeni wa kutaka kujiondoa katika Jumuiya hiyo.

“Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mheshimiwa Bernard Membe, alinukuliwa akisema kuwa nchi yetu inachokisubiri ni talaka tu kutoka kwa washirika wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Kwa nini tukae na kusubiri talaka, kwa nini tusichukue hatua na kuipata Talaka EAC?” alihoji.

Hata hivyo, Mheshimiwa Mbowe alikosoa mtazamo wa wabunge wenzake akionya kuwa hatua ya Tanzania kujitoa itakuwa na athari hasi kwa wananchi wa Tanzania na Afrika Mashariki.

“Ninawaomba wanasiasa wenzangu kujizuia kutoa maneno yanayoweza kuyaumiza mataifa mengine; wajizuie kutoa matamko yanayoweza kuleta wasiwasi wa kidiplomasia kati yetu (Tanzania) na nchi nyingine,” alisema Mheshimiwa Mbowe.

Kwa mujibu wa Mheshimiwa Mbowe, Tanzania na wanachama wengine wa EAC wanatakiwa kujikita katika mazungumzo ya kidiplomasia ili kutafuta sulushisho la mkwamo wa sasa unaoikabili Jumuiya hiyo.

“Sisi (Tanzania) tumekuwa tukisifiwa kama miongoni mwa nchi zenye uwezo mkubwa sana wa kidplomasia duniani, sasa ninashangaa kinachotutokea sasa,” alisema kiongozi huyo wa kambi rasmi ya Upinzani.

Akijibu hoja mbalimbali za wabunge, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta alibainisha kuwa haikuwa sahihi kwamba Tanzania itaondolewa katika Jumuiya hiyo.

Waziri Sitta pia alieleza kuwa Tanzania ambayo imekuwa ikitengwa na washirika wake wa Jumuiya hiyo, inafanya mpango wa kuwa na uhusiano madhubuti wa kiuchumi na kibiashara na nchi za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).



CHANZO: THE CITIZEN
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment