TALIBAN WADAIWA KUHUSIKA NA SHAMBULIZI KWENYE UWANJA WA NDEGE WA KARACHI

karachi1.jpg
Moto mkubwa kwenye Uwanja wa Kimataifa wa Jinnah mjini Karachi Pakistan baada ya wanamgambo wa Kitaliban kuushambulia usiku wa kuamkia leo.


Usiku wa kuamkia leo wanamgambo waliuvamia uwanja wa ndege mkubwa zaidi nchini Pakistan na watu wasiopungua 26 wameripotiwa kuuawa katika mapigano ya usiku kucha.

Shambulizi hilo kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jinnah mjini Karachi, mji ambao ni kitovu cha uchumi wa Pakistan wenye wakazi milioni 18, limetokea huku serikali ya Waziri Mkuu wa nchi hiyo Nawaz Sharif ikijaribu kufanya mazungumzo na wapiganaji wa Taliban kwa lengo la kukomesha mapigano yaliyodumu kwa miaka mingi.

Shambulizi hilo lilianza majira ya saa 5 usiku kwa majira ya Afrika Mashariki baada ya wanamgambo 10 waliovaa sare za jeshi walipoingia kupitia lango la zamani la uwanja huo linalotumiwa na watu maalumu.

Kundi la Taliban nchini Pakistan, ambalo ni muungano wa makundi yanayopigana kuiangusha serikali ya Pakistan, limeripotiwa kudai kuhusika na shambulizi hilo kwa kile ilichokieleza kuwa ni ulipizaji kisasi dhidi ya mashambulizi yanayofanywa na jeshi la serikali dhidi ya ngome zao kwenye mpaka wa nchi hiyo na Afghanistan.

“Huu ni ujumbe wa serikali ya Pakistan kuwa bado tuko hai na ni jibu dhidi ya mauaji ya watu wasiokuwa na hatia katika mashambulizi ya mabomu yanayofanywa na serikali kwenye vijiji vyao,” alisema Shahidullah Shahid, msemaji wa kundi la Taliban.

Shambulizi hilo linaonekana kuwa pigo kubwa dhidi ya serikali ya Sharif ambaye aliingia madarakani kwa ahadi ya kufanya mazungumzo ya amani ili kupata suluhu ya ghasia za miaka mingi nchini humo.

Katika uwanja wa ndege mapigano yaliendelea kwa muda wa saa tano na picha za televisheni zilionesha moto mkubwa huku magari ya wagonjwa yakifanya kazi ya kuondoa majeruhi. Kwa uchache milipuko mitatu mikubwa ilisikika wakati wanamgambo waliovaa mabomu walipojilipua.

Leo asubuhi jeshi lilidai kuwa uwanja huo ulikuwa salama lakini moshi mkubwa ulionekana ukifuka juu ya jengo la uwanja huo.

Msemaji wa jeshi amenukuliwa akisema kuwa wanamgambo kumi wenye umri kati ya 20 na 25 wameuawa na vikosi vya jeshi huku kiasi kikubwa cha silaha na risasi kikipatikana kutoka kwa wapiganaji hao.

Taarifa ya jeshi inasema kuwa washambuliaji hao wana asili ya nchi ya Uzbekistan. Maafisa wa Pakistan wamekuwa wakiwalaumu wapiganaji wa kigeni wanaopewa mafunzo katika eneo la mpaka wa nchi hiyo na Afghanistan ambao wanadaiwa kupambana upande wa Taliban.

Wakati wa shambulizi hilo safari zote za ndege katika uwanja huo zilikuwa zimezuiwa na hakuna taarifa za ndege yoyote kuharibiwa.

Mazungumzo ya amani kati ya serikali na wapiganaji wa Taliban nchini humo yameshindwa katika miezi ya hivi karibuni na hivyo kuua matumaini ya kupatikana suluhu ya uasi unaoikabili nchi hiyo kwa muda mrefu.

Taliban wa Pakistan ni washirika wa Taliban wa Afghanistan.


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment