Mazungumzo ya Kerry na viongzo wa nchi hiyo yatajikita kwenye hatua zitakazochukuliwa na Marekani kuisadia serikali ya al-Maliki kukabiliana na waasi.
|
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani, John Kerry,
leo amewasili mjini Baghdad katika ziara inayolenga kudurusu kuendelea kuzorota
kwa mzozo wa Iraq.
Kerry amepanga kukutana na Waziri Mkuu Nuri al-Maliki na
viongozi wengine wakuu kutoka katika makundi mbalimbali ya kisiasa nchini humo.
Mazungumzo ya Kerry na viongzo wa nchi hiyo yatajikita
kwenye hatua zitakazochukuliwa na Marekani kuisadia serikali ya al-Maliki
kukabiliana na wapiganaji wa kundi la Dola ya Kiislamu katika Iraq na Sham
(ISIS).
Jana Makamu wa zamani wa Rais wa Marekani Dick Cheney aliitaka
Marekani iingilie kijeshi Iraq kwa mara nyingine huku akizikosoa sera za Rais Barack
Obama kuelekea nchi hiyo.
Katika mahojiano kwenye kipindi cha “This Week” kinachorushwa
na kituo cha televisheni cha ABC, Cheney aliutuhumu utawala wa Rais Obama kuwa
unaelewa kitisho cha wapiganaji hao lakini haukufanya vya kutosha kukabiliana
nao.
Kwa siku kadhaa sasa, askari wa jeshi la Iraq wamekuwa
katika mapambano makali na wapiganaji wa ISIS, ambao wametishia kuitwaa miji
mingine ya nchi hiyo ukiwemo mji mkuu, Baghdad.
Wapiganaji hao wameshaitwaa baadhi ya miji muhimu kaskazini
mwa nchi hiyo kama vile mji wa Mosul, ambao ni mji wa pili kwa ukubwa, na mji wa
Tikrit aliozaliwa aliyekuwa kiongozi wa nchi hiyo marehemu Saddam Hussein.
Wiki jana Rais Obama alisema kuwa angetuma wakufunzi 300
wa kijeshi kwenda kuisaidia serikali ya Iraq kukabiliana na ISIS. Pia alisema
kuwa anafikiria kuagiza kufanyika kwa mashambulizi ya ndege.
Kerry anakuwa Ofisa wa kwanza wa ngazi ya juu wa Marekani
kuitembelea Iraq tangu mzozo huo ulipoanza wiki mbili zilizopita.
Amewasili Baghdad ikiwa ni kituo chake cha tatu katika
ziara yake ya Mashariki ya Kati baada ya kuzitembelea Misri na Jordan.
0 comments:
Post a Comment