Mataifa saba yanayoongoza kwa viwanda duniani
yajulikanayo kama “G7” yametishia kuzidi kuibana Urusi kwa kuiwekea vikwazo
zaidi kutokana na mgogoro wa Ukraine.
Katika taarifa iliyotolewa jana Jumatano, G7 inayoundwa na
nchi za Marekani, Canada, Ujerumani, Ufaransa, Uingereza, Japan na Italia,
ziliitaka Moscow kuacha harakati za kuivuruga Ukraine au la ikabiliwe na
vikwazo zaidi.
Taarifa hiyo iliyotolewa kufuatia mkutano wa viongozi wa
mataifa hayo mjini Brussels ilisema kuwa vitendo vya kulivuruga eneo la mashariki
mwa Ukraine havikubaliki na vinapaswa kukoma mara moja.
"Tuko tayari kuongeza vikwazo maalumu na kuchukua
hatua kubwa zaidi za kuitia hasara Urusi iwapo hali italazimu kufanya hivyo,”
ilisema taarifa hiyo.
Akizungumzia vikwazo vya kibiashara, fedha na nishati,
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel alizidi kuionya Urusi dhidi ya vikwazo
vinavyoweza kuiandama akisema: "Hatuweza kuendelea kuvumulia matendo ya
kuivuruga Ukraine. Iwapo hakutakuwa na hatua za utatuzi, kuna uwezekano wa
vikwazo, na hata awamu ya tatu ya vikwazo vikubwa zaidi.”
Mivutano kati ya Urusi na nchi za Magharibi iliongezeka
baada ya eneo la peninsula ya Crimea kwenye Bahari Nyeusi kujiunga na Urusi
kufuatia kura ya maoni iliyofanyika Machi 16 mwaka huu.
Marekani na Jumuiya ya Ulaya zinaituhumu Urusi kuwa
inaivuruga Ukraine. Zimeshaweka vikwazo vya usafiri dhidi ya maafisa na Benki
za Urusi ikiwa ni pamoja na kuzia mali zao.
Hata hivyo, Urusi inazikanusha shutuma hizo na kusema
kuwa maandamano katika eneo la Mashariki mwa Ukraine yalianza kufanyika mapema
kuipinga serikali mpya ya Kiev.
Maandamano ya wanaharakati wanaoegemea upande wa Urusi
yanaendelea katika mikoa ya Donetsk na Luhansk mashariki mwa Ukraine, ambapo
wananchi wa mikoa hiyo walipiga kura ya kijitenga na Kiev.
0 comments:
Post a Comment